Madaraka Dei 2026: Ruto alivyovua kofia kuheshimu Wimbo wa Taifa
DAKIKA chache baada ya kuwasili Wajir Stadium ambako maadhimisho ya Madaraka Dei 2026 yamefanyika Jumatatu, Juni 1, Rais William Ruto alikagua gwaride la heshima lililoandaliwa na vikosi vya pamoja vya majeshi ya Kenya (KDF).
Kwenye maadhimisho mengi ya sikukuu nchini, kwa kawaida kiongozi wa taifa aliye madarakani huvalia suti iliyonyooka na kuyaongoza.
Mojawapo ya itifaki zinazofuatwa, ni wimbo wa taifa hata kabla ya wimbo wa taifa kuchezwa.
Kwenye maadhimisho ya Madaraka Dei 2026, Dkt Ruto na masafara wake wa ulinzi aliingia uwanja wa Wajir akiwa amevalia suti maalum aina ya Kaunda ya rangi nyeupe. Hali kadhalika, kiongozi wa nchi aliyeonekana maridadi akiwa amevalia kofia nyeupe ya mviringo inayojulikana kama “god father”.
Rais Ruto, akipungia wananchi mikono aliingia kwa karandinga ya jeshi akiwa pamoja na Mkuu wa Majeshi ya Kenya Jenerali Charles Kahariri.
“Tunaomba wasio na kofia rasmi wazivue kwa sababu ya wimbo wa taifa,” alisema mfawidhi wa sherehe kutoka KDF. Kinyume na ilivyotarajiwa, sawa na wanachi, Rais Ruto alivua kofia yake huku anga ya Wajir Stadium ikitwaliwa na Wimbo wa Taifa na ule wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, mtawalia.
Itifaki ya kawaida ya gwaride la heshima la Rais ni kama ifuatavyo: Wimbo wa Taifa ambapo Rais huwasili, anapokea salamu za heshima za kijeshi na kusimama kwa umakini huku Wimbo wa Taifa ukichezwa. Ukaguzi wa Kikosi cha Heshima, baada ya Wimbo wa Taifa kumalizika, Rais huandamana na kamanda wa kikosi hicho (au Mkuu wa Majeshi) kukagua Kikosi cha Heshima.
Itifaki zote hizo, Rais Ruto alizifuata. Kwa kawaida, katika shughuli rasmi za Serikali, Wimbo wa Taifa huimbwa au kupigwa kwa ala za muziki beti moja tu pamoja na kiitikio chake.