HabariHabari za Kitaifa

Mgomo wa mafuta ya petroli: Dada wawili wauza bendera kuwapa motisha wahudumu wa matatu   

May 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MGOMO wa kitaifa wa wahudumu wa matatu dhidi ya bei ghali ya mafuta ya petroli ukiendelea mnamo Jumatatu, May 18, 2026, dada wawili katika Kaunti ya Nairobi walijitokeza kuwapa motisha waandamanaji kwa njia ya kipekee.

Salome Muchungu na Ann Muchungu, ambao ni wakazi wa mtaa wa Kasarani walitua kwenye barabara kuu ya Thika – Nairobi, maarufu kama Thika Superhighway, kuuza bendera ya Kenya katika kile walichohoji ni ushirikiano na Wakenya kutaka bei ya mafuta ishushwe.

“Maisha yamekuwa magumu, tunataka bei ya mafuta ya petroli ipunguzwe tuweze kulea familia zetu bila mahangaiko,” waliambia Taifa Dijitali. Walisema walichagua kuuza bendera kwa sababu ndio nembo ya taifa, na ilionyesha ushirikiano na umoja kwa ajili ya gharama ya juu ya maisha ‘kwa kiasi kikubwa kuchochewa na mfumko wa bei ya mafuta ya petroli’.

Dada wawili, Ann Muchungu na Salome Muchungu wakichuuza bendera mnamo Jumatatu, Mei 18, 2026 Thika Road wakati wa maandamano ya wahudumu wa matatu dhidi ya kupanda kwa bei ya mafuta ya petroli. Wanasema hatua ya kuuza bender ani ishara ya kuwapa motisha wahudumu wa matatu na ushirikiano. Picha|Sammy Waweru

Tunaonyesha ushirikiano na umoja kwa Wakenya wenzetu – wahudumu wa matatu, bei ya mafuta ya petroli yapunguzwe, walisisitiza. Walipoulizwa wangetaka ishushwe hadi kiwango kipi, walitumia mfano wa nauli ambayo wamekuwa wakilipa kutoka Kasarani hadi Nairobi kuelekea kazini.

“Waume zetu, kila mmoja akitupa Sh200 kuenda kazini kisha nauli iwe Sh100 kwenda jijini Nairobi pekee hatutasalia na pesa zozote za kununulia watoto chakula,” wakasema. Ann, ni mama wa mtoto mmoja huku dada yake, Salome amejaaliwa na watoto wawili.

Uchukuzi na usafiri wa umma ulitatizika mnamo Jumatatu kufuatia mgomo wa kitaifa nchini, uliotishwa na miungano ya wamiliki na wahudumu wa matatu, magari ya kibinafsi, teksi na bodaboda.

Wanapinga kupanda kwa bei ya mafuta ya petroli, ambapo Mamlaka ya Kudhibiti Kawi na Petroli (EPRA) mnamo Alhamisi, Mei 14, 2026 ilitathmini bei itakayotumika kati ya Mei hadi Juni 14.

Ann Muchungu akichuuza bendera mnamo Jumatatu, Mei 18, 2026 Thika Road wakati wa maandamano ya wahudumu wa matatu dhidi ya kupanda kwa bei ya mafuta ya petroli. Picha|Sammy Waweru

EPRA iliongeza bei ya dizeli kwa Sh46.29 kwa lita, huku bei ya petroli ikiongezeka kwa Sh16.65 kwa lita. Hivyo basi, petroli sasa inauzwa Sh214.25 kwa lita na dizeli kwa Sh242.92, huku bei ya mafuta ya taa ikisalia Sh152.78.

Ni nyongeza ambayo tayari athari zake zimeanza kushuhudiwa haswa kwa nauli, chakula na mahitaji mengine muhimu ya kimsingi. Maafisa wa polisi na wale wa kukabiliana na ghasia, katika maeneo tofauti nchini walikabiliwa na kibarua kigumu kufungua barabara.

Thika Super Highway, kwa mfano, Jumatatu asubuhi ilisalia kufungwa Wakenya wengi wanaofanya kazi jijini Nairobi na mitaa mingine wakitatizika kuripoti gangeni.