Makala

Onyo la mvua kubwa sehemu kadhaa nchini wikendi

Na BENSON MATHEKA March 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Idara ya Hali ya Hewa nchini imetoa tahadhari kwa Wakenya wanaoishi katika maeneo mbalimbali kujitayarisha kwa mvua ya wastani hadi kubwa kwa muda wa siku tano zijazo.

Katika taarifa ya hali ya hewa ya mwishoni mwa wiki iliyotolewa Ijumaa, Machi 13, idara hiyo ilisema mvua inatarajiwa kunyesha katika maeneo ya Magharibi mwa Kenya, Nyanda za Juu za Kati, Bonde la Ziwa Victoria, Bonde la Ufa na maeneo ya Kusini-mashariki mwa nchi.

Katika maeneo ya Magharibi, Bonde la Ufa na Bonde la Ziwa Victoria, kaunti zinazotarajiwa kupokea mvua ni Siaya, Kisumu, Homa Bay, Migori, Kisii, Nyamira na Trans Nzoia.

Kaunti nyingine ni Baringo, Uasin Gishu, Elgeyo Marakwet, Nandi, Nakuru, Narok, Kericho, Bomet, Kakamega, Vihiga, Bungoma, Busia na West Pokot.

Kwa mujibu wa idara hiyo, maeneo haya yatapokea mvua kubwa hasa nyakati za alasiri, huku mvua hiyo ikitarajiwa kuandamana na radi na ngurumo.

Mvua hizo za alasiri zitafuatia manyunyu mepesi ya asubuhi na vipindi vya jua katikati ya asubuhi. Idara hiyo pia ilisema baadhi ya maeneo yanaweza kushuhudia mvua wakati wa usiku.

Hali kama hiyo ya mvua inatarajiwa pia katika kaunti za Nyanda za Juu za Kati ikiwemo Nyandarua, Laikipia, Nyeri, Kirinyaga, Murang’a, Kiambu, Meru, Embu, Tharaka Nithi pamoja na Nairobi.

Wakazi wa maeneo haya wameonywa kujitayarisha kwa mvua kubwa kuanzia Ijumaa hadi Jumamosi, huku kiwango cha mvua kikitarajiwa kupungua kidogo katika siku zinazofuata ndani ya kipindi hicho cha utabiri.

Wakati huo huo, idara hiyo ilisema maeneo ya nyanda za chini kusini-mashariki kama Kitui, Makueni, Machakos, Kajiado na Taita Taveta pamoja na sehemu za bara za kaunti ya Tana River zitapokea manyunyu mepesi.

Mbali na mvua zinazoendelea kunyesha katika sehemu nyingi za nchi, idara hiyo pia imeonya wakazi wa Nyanda za Juu za Kati kujitayarisha kwa baridi kali wakati wa usiku.

Kwa mujibu wa utabiri huo, kaunti za Nyandarua, Laikipia, Nyeri, Kirinyaga, Murang’a, Kiambu, Meru, Embu, Tharaka Nithi na Nairobi zitashuhudia baridi kali usiku huku halijoto ikishuka hadi nyuzi joto 9°C kabla ya kupanda kidogo hadi takriban 11°C mwishoni mwa kipindi cha utabiri.

Kwa upande mwingine, kaunti za Kaskazini Mashariki za Wajir, Mandera, Garissa, Isiolo na Marsabit zinatarajiwa kushuhudia joto kali mchana likifikia hadi nyuzi joto 38°C katika siku tano zijazo.