Habari Mseto

Nuru Okanga, Jakababa wataka waachiliwe ‘kwa sababu Raila ameungana na Serikali’


WAFUASI wawili sugu wa kinara wa chama cha ODM Raila Odinga wameomba mahakama itamatishe kesi za uchochezi zinazowakabili baada ya kiongozi huyo wa Azimio la Umoja One kuungana na Serikali ya Rais William Ruto.

Mabw Nuru Okanga na Omosh Jakababa walimsihi hakimu mwandamizi Geoffrey Onsarigo atamatishe kesi za uchochezi dhidi yao.

“Twaomba kesi zinazotukali zifutiliwe mbali kufuatia Raila kuungana na serikali ya Rais Ruto,” Okanga na Jakababa walimsihi hakimu.

Wawili hao walieleza mahakama Raila aliitaka serikali itamatishe kesi za kisiasa dhidi ya wote waliopinga serikali ya Kenya Kwanza kutokana na maongozi mabaya.

Lakini hakimu hakutamatisha kesi dhidi ya wawili hao akisema “mkurugenzi wa mashtaka ya umma –DPP-Renson Ingonga hajatoa mwelekeo.”

Wawili hao wamekana mashtaka ya uchochezi dhidi ya serikali ya Rais Ruto.