Siasa chafu Nyanza sasa zakera wakazi
MIJADALA ya kisiasa katika eneo la Nyanza inazidi kushuka hadhi huku baadhi ya viongozi wakitumia lugha chafu, matusi ya kingono na matamshi ya kudhalilisha kuwashambulia wapinzani wao kisiasa.
Mtindo huo ambao umeongezeka kwa kasi katika kipindi cha mwaka mmoja uliopita, umeacha wapigakura wengi wakihisi kutengwa, kuaibika na kukerwa sana.
Baadhi ya wakazi wanasema hawawezi tena kuhudhuria mikutano ya kisiasa pamoja na familia zao kwa kuhofia lugha inayotumiwa na viongozi majukwaani.
Eneo hilo ni ngome ya chama cha Orange Democratic Movement (ODM), lakini migawanyiko ya ndani ya chama hicho imegeuka kuwa ya kibinafsi, yenye uchungu na mashambulizi makali.
Mnamo Februari 26, 2026, serikali ya Kaunti ya Siaya ilimfuta kazi Afisa wa Usimamizi wa Habari, Richard Omondi maarufu kama Makamu wa Makamu.
Barua ya kufutwa kazi ilisema Bw Omondi alitoa matamshi yasiyofaa, ya kudhalilisha, ya matusi na yasiyo ya heshima dhidi ya bosi wake, Gavana wa Siaya James Orengo.
Tukio hilo lilitokea siku moja kabla ya mkutano wa kisiasa, Kaunti ya Kisumu.
Bw Omondi alimshutumu Gavana Orengo, Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino kwa kuacha mrengo wa Linda Ground na kujiunga na kundi la Linda Mwananchi kwa sababu za kingono.
Kauli hizo zilitolewa mbele ya viongozi wakuu wa ODM akiwemo mwenyekiti wa chama hicho na Gavana wa Homa Bay Gladys Wanga pamoja na Seneta wa Kisumu Tom Ojienda.
Siku iliyofuata, Bw Omondi alipokea barua ya kusimamishwa kazi kutoka serikali ya kaunti.
“Ofisi hii imefahamishwa kuhusu tukio lililotokea wakati wa shughuli ya kisiasa ndani ya Kaunti ya Kisumu mnamo Februari 25 ambapo ulitoa matamshi yasiyofaa, ya kudhalilisha, ya matusi na yasiyo ya heshima dhidi ya Gavana wa Siaya,” sehemu ya barua hiyo ilisoma.
Hata hivyo, miezi mitatu baadaye, Mei 18, 2026, Bw Orengo mwenyewe alijipata katikati ya mjadala kama huo baada ya kutumia lugha ya kuudhi katika mkutano wa kisiasa mjini Oyugis, Kaunti ya Homa Bay.
Akizungumza na wafuasi wake, alimlenga Bi Wanga, ambaye pia ni mwenyekiti wa ODM. Alianza kwa kupuuza kulinganishwa kisiasa na gavana huyo.
“Mimi ni mwanasiasa ambaye hapaswi kuchezewa. Nimeona siasa tofauti na alizopitia,” alisema kwa Dholuo.
Kisha akaingia katika matamshi ya wazi ya kingono huku akisisitiza kuwa bado ana nguvu kisiasa licha ya kukosolewa kwa umri wake.
Kauli hizo zilienea kwa kasi katika mitandao ya kijamii na kuzua ukosoaji mkubwa pamoja na wasiwasi kuhusu kuzorota kwa mazungumzo ya kisiasa katika eneo hilo.
Watumiaji wengi wa mitandao walilalamika kuwa mikutano ya kisiasa Nyanza imejaa lugha chafu kiasi kwamba wazazi hawawezi tena kuhudhuria kwa utulivu wakiwa na watoto wao.
Wakati huo huo, wanawake wabunge wa kaunti ya Kisumu wamemtaka lBw Orengo kuomba radhi kwa wanawake wa Kenya na kwa Bi Wanga kwa matamshi yake.
“Bw Orengo lazima awaombe radhi wanawake wa Kenya na Gavana Gladys Wanga kwa kukiuka Katiba na kudhalilisha afisi anayoshikilia,” alisema Bi Okombo.
Mbunge wa Suba Kaskazini, Bi Millie Mabona, pia alikosoa mwenendo huo kupitia ukurasa wake wa mitandao ya kijamii.
“Ninachukia aina ya siasa katika eneo langu. Tukitofautiana tufanye hivyo kwa heshima. Aliyelala nawe hawezi kumsaidia mwananchi wa kawaida,” aliandika.
Mchambuzi wa siasa Profesa Amukowa Anangwe , alisema ubora wa siasa nchini umeshuka sana katika miaka ya hivi karibuni.
“Siasa sasa zimekuwa uwanja wa wahuni, wawe wafanyabiashara wa dawa za kulevya, matapeli, waabudu shetani na wahalifu wa kila aina,” alisema.
Profesa Anangwe alisema lugha chafu na ukosefu wa maadili katika siasa ni dalili ya tatizo kubwa zaidi katika jamii.
Huko Kisumu, Bunge la Wananchi limemtaka Bw Orengo kuomba radhi hadharani kwa Bi Wanga kutokana na matamshi yake ya kudhalilisha.
Wakati huo huo, wanawake wabunge wa kaunti ya Kisumu wametaka Baraza la Magavana kuandaa kikao cha dharura kupatanisha viongozi hao wawili.
Wakiongozwa na Naibu Spika wa Bunge la Kaunti ya Kisumu na MCA wa Manyatta B, Bi Nereah Okombo, viongozi hao walimtaka Bw Orengo kuomba radhi kwa wanawake wa Kenya na kwa Bi Wanga.
“Bw Orengo lazima awaombe radhi wanawake wa Kenya na Gavana Gladys Wanga kwa kukiuka Katiba na kudhalilisha afisi anayoshikilia,” alisema Bi Okombo.