Sababu za mahakama kufuta uteuzi wa Jumwa kusimamia bodi ya barabara
MAHAKAMA Kuu imefuta uteuzi wa aliyekuwa Waziri Aisha Jumwa kuwa mwenyekiti wa Bodi ya Barabara Kenya ikisema kuwa mchakato uliotumika ulikiuka sheria zinazosimamia uteuzi katika moja ya taasisi muhimu za miundombinu nchini.
Mahakama hiyo pia ilikataa hoja ya serikali kwamba Bi Jumwa aliteuliwa katika bodi hiyo na Chama cha Wasafirishaji Kenya (KTA) mojawapo ya mashirika ya wadau yanayotambuliwa kisheria, kabla ya Rais kumteua kuwa mwenyekiti.
Katika uamuzi huo unaoangazia uteuzi kwa misingi ya kisiasa serikalini, mahakama ilisema hakuna ushahidi wa kuonyesha kuwa utaratibu wa kisheria ulifuatwa kikamilifu.
Kwa msingi huo, ilitangaza kuwa uteuzi wa Bi Jumwa ulikuwa “kinyume cha Katiba na batili tangu mwanzo”.
Mahakama ilisema uteuzi huo haukuzingatia Kifungu cha 7 cha Sheria ya Bodi ya Barabara Kenya na masharti ya Katiba kuhusu uadilifu, haki ya utawala bora na uteuzi wa watumishi wa umma kwa kuzingatia sifa.
Kifungu hicho kinaeleza muundo wa bodi hiyo na kinahitaji wanachama wake kutoka taasisi maalum za kitaaluma na wadau wa sekta ya barabara na usafiri.
Pia, kinamtaka Rais kumteua mwenyekiti kutoka miongoni mwa wanachama walioteuliwa kwa njia hiyo, jambo linalomaanisha lazima pawe na mchakato wa uteuzi unaohusisha mashirika husika.
“Uteuzi wa Bi Jumwa kuwa mwanachama wa Bodi ya Barabara Kenya ni kinyume cha Katiba na batili tangu mwanzo kwa kuwa haukuzingatia Kifungu cha 7 cha Sheria ya Bodi ya Barabara Kenya na Ibara za 10, 47 na 232 za Katiba ya Kenya ya 2010,” mahakama ilisema.
Mahakama pia ilielekeza kuwa uteuzi wowote mpya lazima uzingatie kikamilifu Sheria, Katiba na kanuni za utumishi wa umma.
Kesi hiyo iliwasilishwa na mwanaharakati Francis Awino, aliyedai kuwa Bi Jumwa aliteuliwa bila kufuata utaratibu wa kisheria unaohitajika.
Pia kulikuwa na kesi nyingine zilizowasilishwa na Chama cha Wanasheria Kenya (LSK) na mtetezi wa haki Patrick Njuguna, zote zikipinga uteuzi huo.
Kulingana na stakabadhi za mahakama, Bi Jumwa aliteuliwa kwanza kuwa mwanachama wa bodi kupitia tangazo la Gazeti la Serikali Nambari 384 la Januari 16, 2025, kabla ya Rais kumteua kuwa mwenyekiti siku iliyofuata kupitia tangazo Nambari 395 la Januari 17, 2025.
Hata hivyo, walalamishi walisema sheria inahitaji mwenyekiti achaguliwe kutoka kwa wanachama waliopendekezwa na taasisi zilizotambuliwa kisheria.
Baadhi ya taasisi hizo ni Taasisi ya Wahandisi Kenya, Chama cha Wamiliki wa Magari, Chama cha Watengenezaji Kenya, Taasisi ya Wahasibu Waliothibitishwa na Chama cha Wasafirishaji Kenya.