Habari za Kitaifa

Moyo wangu uko tayari kwa Afrika, asema Raila

Na BENSON MATHEKA August 27th, 2024 1 min read

MGOMBEAJI wa Kenya wa kiti cha Mwenyekiti wa Tume ya Muuungano wa Afrika (AUC) Raila Odinga amesema yuko tayari kwa wadhifa huo anaonuia kuunganisha bara nzima.

“Niko tayari, moyo wangu uko tayari kuhudumia Bara la Afrika na kuendeleza ajenda na malengo ya waanzilishi wa Afrika huru,” Bw Odinga aliambia marais na viongozi waliohudhuria hafla ya kumzindua kama mgombeaji wa Kenya.

Alisema ana ufahamu mkubwa wa Muungano wa Afrika kutokana na tajiriba yake kama mpatanishi na Mjumbe wa AU kuhusu miungomsingi.

Alisema kuwa kuungwa mkono na Afrika Mashariki kunatia nguvu azma yake na akaahidi kutovunja moyo viongozi na wakazi wa Afrika Mashariki.

Waziri Mkuu huyo wa zamani alisema hayo Jumanne, Agosti 27, 2024 wakati wa kuzinduliwa rasmi kwa safari yake kuanza kampeni kuwania uenyekiti wa AUC, katika Ikulu, Nairobi.

Rais William Ruto alizindua rasmi safari hiyo katika hafla iliyohudhuriwa na marais na viongozi kadha kutoka Ukanda wa Afrika Mashariki.

Waliohudhuria ni pamoja na Rais Yoweri Museveni wa Uganda, Samia Suluhu (Tanzania), Salvar Kiir (Sudan Kusini).

Marais wastaafu waliokuwepo ni Bw Olusegun Obasajo (Nigeria) na Jakwaya Kikwete(Tanzania), miongoni mwa wengine

Bw Odinga aliahidi kuunda baraza la mawaziri wa kumsaidia kuendeleza ajenda zake kuhusu Bara la Afrika litakalokuwa na wawakilishi kutoka pande zote za Afrika.