Habari Mseto

Mlinzi auawa shuleni gari la mwalimu likiibwa

Na GEORGE MUNENE September 21st, 2024 1 min read

MLINZI katika Shule ya Upili ya Kibirigwi, Kaunti ya Kirinyaga, aliuawa na wezi waliovamia shule hiyo Ijumaa usiku, Septemba 20, 2024.

Walinzi wengine watatu na msimamizi wa walimu walifungwa kamba na wezi hao ambao walivunja afisi za shule hiyo kisha kuiba kiasi cha pesa kisichojulikana.

Vitu vya dhamana na pia gari la mwalimu mmoja, viliibwa.

Hata hivyo, gari hilo lilipatikana katika eneo la Kabati, Kaunti ya Murang’a baada ya kuwachwa na wezi hao njiani.

Kulingana na Kamshina wa Kaunti ya Kirinyaga Bw Allasow Hussein, tukio hilo lilitokea wakati wanafunzi walikuwa wamelala.

“Tukio hili lilikuwa limepangwa. Maafisa wa usalama watashughulikia hadi kuwakamata wezi hao,” alisema Bw Hussein.