Jinsi mawakili walivyosimama na mwanaharakati Njeri
ALIYEKUWA Jaji Mkuu David Maraga na mwanasheria mwenye tajriba ya juu (SC) Kalonzo Musyoka na mawakili zaidi ya 30 walisimama na mwanaharakati Rose Njeri akishtakiwa kwa kuvuruga mtandao wa Mswada wa Fedha wa 2025/2026.
Jaji Maraga , SC Musyoka na mawakili chungu nzima wakiongozwa na wakili mkongwe Dkt John Khaminwa , Eric Theuri , Daniel Maanzo na Kibe Mungai walimweleza hakimu mwandamizi Geoffrey Onsarigo kuwa mashtaka mawili dhidi ya Njeri “hayana mashiko kisheria na yanafaa kufutiliwa mbali.”
Bw Onsarigo alifahamishwa kwamba Njeri anashtakiwa kwa kuitikia mwito wa Bunge kutoa maoni kuhusu Mswada wa Fedha 2025/2026.
Akasema Jaji Maraga , “Inashangaza kabisa Njeri anashtakiwa kwa kuitikia mwito wa bunge.”
Bw Musyoka alieleza mahakama kwamba “hii serikali haina aibu kwa kumkamata Njeri kwa kutii wito wa Bunge kutoa maoni kuhusu mswada wa fedha wa 2025/2026 ndipo maoni hayo yashirikishwe katika mswada huo.”
Mabw Theuri ,Mungai na Dkt Khaminwa walimsihi hakimu apuuze kesi hiyo kwa vile inakandamiza haki za mshtakiwa za kutoa maoni na kujieleza.
Mahakama ilielezwa “ni aibu kwa serikali kukandamiza haki za wakenya kwa kuharamisha maoni yao na kuwatia nguvuni.”
Hakimu aliombwa atumie mamlaka na uwezo aliopewa na sheria kuzima hatua ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) Renson Ingonga kukaidi sheria na katiba kwa kufutilia mbali kesi dhidi ya Njeri.
Bw Theuri alieleza mahakama kwamba yasikitisha Njeri alitiwa nguvuni Ijumaa na kuzuiliwa kwa siku nne bila sababu.
Mahakama ilielezwa Njeri hajafanya makosa na kila mmoja anashangaa alifikishwa kortini kufanya nini na mahakamani sio mahala pa kutembelea ovyo ovyo na wala sio bustani ya Uhuru Park.
“Achilia mshtakiwa kwa dhamana. Amuru asijibu shtaka na uamuru tuwasilishe rasmi ombi la kupinga kushtakiwa kwa Njeri,” Bw Mungai alimsihi hakimu.
Mahakama ilielezwa zaidi kwamba Katiba ya Kenya Kifungu nambari 25 na 31 zimepinga kudhulumiwa kwa wananchi.
Akitoa uamuzi mahakama iliagiza mshtakiwa atie sahihi cheti cha mahakama cha dhamana ya Sh100,000.
Kwa mujibu wa cheti hiki mshtakiwa akikosa kufika kortini atailipa serikali kitita cha Sh100,000.
Mahakama ilisitisha kufunguliwa kushtakiwa kwa Njeri hadi Juni 20,2025 mahakama itakapotoa uamuzi ikiwa mashtaka dhidi ya mwanaharakati huyu ni halali.
Kiongozi wa mashtaka Juma Victor Owiti katika mawasilisho yake alipinga ombi la mshtakiwa la kutupwa kwa kesi hiyo akisema “ameshtakiwa kwa mujibu wa sheria.”