Joho atetea viongozi wanaoenda kupiga magoti ikulu kuomba miradi ya maendeleo
WAZIRI wa Madini na Uchumi wa Baharini Hassan Joho, ametetea ziara za hivi majuzi za viongozi wa chama cha ODM katika Ikulu, akisema hakuna kosa lolote kukutana na Rais William Ruto kujadili masuala ya maendeleo.
Akizungumza jijini Mombasa baada ya kushiriki sala za Idd katika Msikiti wa Ummul Kulthum, Kizingo, Bw Joho alipuuzilia mbali ukosoaji unaoelekezwa kwa viongozi wa Pwani waliokutana na Rais hivi karibuni.
“Kuna ajabu gani kwa kiongozi kuketi na Rais? Kwa nini maswali haya yote? Kuna shida gani sisi kama uongozi wa Pwani kuketi na Rais Ruto? aliuliza.
Bw Joho, ambaye alikuwa Naibu Kiongozi wa zamani wa ODM, alisisitiza kuwa urais ndio kitovu cha maendeleo ya kitaifa, na mikutano kama hiyo ni muhimu ili kuhakikisha maeneo yao yanapiga hatua kimaendeleo
“Kwa nini maswali huulizwa tu viongozi wa Pwani wanapokutana na Rais? Kwa nini hamwaulizi maswali kama hayo viongozi kutoka Siaya au Magharibi mwa Kenya?” aliuliza.
Kauli za Bw Joho zinajiri siku moja baada ya Gavana wa Siaya, James Orengo, kuongoza viongozi kutoka maeneo bunge sita ya kaunti hiyo hadi Ikulu kwa mazungumzo na Rais Ruto.
Matokeo ya mkutano huo yalikuwa ni ahadi ya Rais ya miradi ya maendeleo ya mabilioni ya shilingi katika kaunti ya Siaya, ikijumuisha miundomsingi na sekta nyingine muhimu.
Licha ya mabadiliko yanayoendelea katika kisiasa, Bw Joho alikataa kuzungumzia joto la kisiasa, akisema kwamba kwa sasa kazi yake ni kuhudumia wananchi kupitia wadhifa wake wa uwaziri.
“Tuko mwaka gani sasa? 2025. Barabara zisijengwe hadi 2027? Mimi ni Waziri katika serikali hii. Nina majukumu mahususi katika sekta ya Madini na Uchumi wa Bahari pamoja na masuala ya mabaharia. Niulizeni kuhusu hayo. Siasa nitazungumzia baadaye wakati ufaao,” alisema.
Waziri huyo wa wa Madini na Uchumi wa Bahari alisisitiza kuwa lengo lake ni kutekeleza ajenda ya maendeleo ya serikali ya Kenya Kwanza kikamilifu.
“Sioni joto la kisiasa—naona tu msukumo wa kazi. Ndiyo maana tupo hapa. Sizungumzi kwa niaba ya wengine. Nina kazi nyingi katika wizara yangu,” aliongeza.
Bw Joho pia alitumia nafasi hiyo kuwasihi wakazi wa Mombasa kujisajili kwa ajili ya Mpango wa Makazi Nafuu.
“Nataka kuwaambia wakazi wa Mombasa wajisajili katika Mpango wa Makazi Nafuu. Mumeuona mpango huu ukitekelezwa kote nchini. Usajili kwa mradi wa eneo bunge la Nyali unaendelea. Kutakuwa na nyumba 1,976 pamoja na miundombinu mingine ya kijamii,” alieleza.
Alionya kuwa ikiwa wenyeji hawatajitokeza kujiandikisha, nyumba zilizopangiwa wakazi wa Mombasa huenda zikatolewa kwa watu wengine kutoka maeneo ya nje.