Gavana Nassir achemkia Gachagua kwa njama ya kumfanya ‘wantam’ Mombasa
GAVANA wa Mombasa, Bw Abdulswamad Nassir, amemkashifu aliyekuwa Naibu Rais, Bw Rigathi Gachagua, kwa njama ya kutaka kumng’atua mamlakani ifikapo mwaka wa Uchaguzi Mkuu 2027.
Bw Nassir anatarajia kutetea kiti hicho kwa hatamu ya pili.
Katika ziara yake eneo la Pwani wiki mbili zilizopita, Bw Gachagua alisema anaweka mikakati ili Bw Nassir asipate ushindi katika uchaguzi ujao.
Kulingana naye, mrengo wa upinzani anaouongoza unashirikiana na Mbunge wa Nyali, Bw Mohammed Ali.
Bw Ali ndiye mbunge pekee aliyechaguliwa kupitia chama tawala cha UDA katika Kaunti ya Mombasa, na alikuwa akiegemea upande wa Bw Gachagua alipokuwa naibu rais.
Hata hivyo, tangu Bw Gachagua alipoondolewa mamlakani, Bw Mohamed hajaonyesha wazi anakoegemea.
Aliashiria nia ya kutaka kuhama UDA alipoibua madai ya ulaghai katika uchaguzi wa viongozi wa chama mashinani miezi michache iliyopita.
Mbunge huyo ambaye anahudumu kwa muhula wake wa pili, ni mmoja wa wanaomezea mate ugavana, kando na kaimu katibu mkuu wa UDA, Bw Hassan Omar.
“Majuzi aliyekuwa Naibu Rais alifika hapa Changamwe akasema amenipangia. Amenipangia yeye na nani? Bw Gachagua, hata uje na jeshi lako lote, mimi nina dua na radhi za wazee wangu na nina kura za watu wa Mombasa,” alisema.
Bw Nassir alipuuzilia mbali kauli za Bw Gachagua kwamba Wapwani ni binamu zake.
“Alipokuwa mamlakani si alisema hatuna hisa kwa serikali kwa sababu chama chetu ni ODM? Alisahau? Ghafla bin vu wamekuwa watetezi wa bandari?” aliuliza Bw Nassir alipokuwa kwenye hafla ya elimu Changamwe.
Bw Nassir aliwafokea wapinzani wake kwa kumkejeli akisema ataendelea kuhudumia wakazi wa Mombasa.
“Hata muniite majina gani nitasalia kuwa gavana wa Mombasa na nitahudumia wakazi. Wekeni vikwazo vyovyote na nitawahudumia wakazi,” alisema.
Wakati huo huo, aliwaambia viongozi wa Mombasa wamuunge mkono kuhudumia wakazi ili wapigakura wasiumie kwa sababu ya tofauti zao za kisiasa.
“Mimi nitakuwa na watu, hawa ndio watanilinda. Kama maneno yangekuwa mishale mwili wangu ungekuwa umeshatoboka. Lakini nilitukanwa na kutolewa maneno ambayo hata hayana ukweli kabla niwe gavana. Najua nitaendelea kutukanwa,” alisema Bw Nassir.