Jamvi La Siasa

Wimbi la kusajili vyama kulenga 2027 lashika kasi

Na  MOSES NYAMORI June 18th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

KUNA wimbi jipya la kusajili vyama vya kisiasa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027, hali ambayo imesababisha ongezeko la idadi ya vyama vipya.

Wiki hii, Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa (ORPP) imetoa usajili wa muda kwa vyama vinne vipya vya kisiasa, na kufanya saba idadi ya vyama vilivyosajiliwa tangu mwezi uliopita.

Vyama vilivyosajiliwa upya ni pamoja na Party of Action (Poa), The Economic Pillars Alliance (Tepa), Achievement Party of Kenya (Acpok), na Mkenya Daima Party (MKDP).P

oa imetaja Samuel Macharia, Juma Hemedi, Riziki Ahmed, Lilian Njogu, Sanju Kajwang na Geoffrey Githae kuwa wanachama waanzilishi. Waasisi wa TEPA ni Julius Karanja, Joseph Mwangi, Bennitah Kisongora, na Celine Marongo.

Acpok ilianzishwa na Protas Nyongesa, Joyce Mwangi, na Wilfred Kimathi, huku MKDP ikiwataja John Thuo, Rose Mwalili, na Julius Mghanga kama waanzilishi wake.

Mnamo Mei, vyama saba vya kisiasa vilipokea usajili wa muda huku vingine vitano vikiwa katika mchakato wa kupata usajili kamili.Vilivyosajiliwa kwa muda mwezi Mei ni pamoja na Peoples Forum for Rebuilding Democracy, Imarisha Uchumi Party, African Development Congress, na Kenya Ahadi Party ambavyo viliorodheshwa mara ya kwanza mwezi Machi.

Vyama vingine vipya ni pamoja na National Economic Development Party, Forum for Economic Development Agenda (FEDA) na Kenya United Generation Party.

Wimbi hili la kusajili vyama vya kisiasa limechangiwa kwa kiasi kikubwa na mabilioni ya pesa zinazotolewa na serikali kwa vyama vya kisiasa, pamoja na hamu ya baadhi ya watu kuingia katika miungano kama vinara washirika.

Baadhi hawasajili vyama kwa lengo la kushiriki moja kwa moja katika kisiasa, bali kwa nia ya kuuza vyama hivyo Uchaguzi Mkuu wa 2027 unapokaribia.Biashara ya kununua na kuuza vyama vya kisiasa imekuwa ikinoga, ikichochewa na hofu ya wanasiasa kunyimwa nafasi katika kura za mchujo ndani ya vyama vikuu.

Wanasiasa kadhaa mashuhuri wamewahi kujikuta bila vyama baada ya makundi hasimu kutwaa vyeti vya vyama. Matukio haya yamewachochea baadhi ya viongozi kuunda na kumiliki vyama vyao kama njia ya kujihakikishia tiketi za kugombea na kushiriki mazungumzo ya miungano.Kupata fedha za umma pia kumefanya umiliki wa chama kuwa na mvuto wa kifedha.

Takriban vyama 48 vya kisiasa vilivyoshiriki katika uchaguzi wa 2022 sasa vinanufaika na fedha za walipa ushuru kufadhili shughuli zao.Vyama vidogo kadhaa ambavyo havijawahi kufadhiliwa na serikali awali sasa vinapata mamilioni ya pesa, kufuatia marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Kisiasa.

Sheria hiyo inaeleza kuwa asilimia 70 ya Hazina ya Vyama vya Kisiasa inatolewa kwa kuzingatia kura zote zilizopigiwa chama husika katika uchaguzi uliopita.

Asilimia 15 zaidi hutolewa kulingana na idadi ya wagombea walioteuliwa kutoka kwa makundi maalum ya kijamii, asilimia 10 kulingana na idadi ya wawakilishi waliochaguliwa kwa chama hicho, huku asilimia 5 iliyosalia ikitengwa kwa gharama za usimamizi wa ORPP.

Masharti haya yanamaanisha kuwa chama chochote cha kisiasa kinachowasilisha wagombea katika Uchaguzi Mkuu kinaweza kufuzu kupata ufadhili wa umma, hata kama wengi wa wagombea wake watashindwa, mradi tu wapate kura za kutosha.

Kwa sasa, Kenya ina jumla ya vyama 90 vya kisiasa vilivyosajiliwa kikamilifu. Kati ya hivyo, ni vyama 48 pekee vilivyoshiriki kikamilifu katika Uchaguzi Mkuu wa 2022