Kimataifa

Ukraine yapokea zaidi ya miili 6,000 ya wanajeshi wake waliouawa vitani

Na MASHIRIKA June 19th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

SERIKALI ya Urusi imeikabidhi Ukraine miili ya zaidi ya wanajeshi wake 6,000 waliouawa vitani, kama sehemu ya makubaliano ya kubadilishana wafungwa.

Kwa mujibu wa Waziri wa Ulinzi wa Ukraine, Rustem Umerov, jumla ya miili 6,057 imeshapokelewa hadi sasa, huku Urusi ikisema imekabidhi jumla ya miili 6,060 — tofauti ndogo ya takwimu ambayo haijafafanuliwa rasmi.

Kwa upande wake, Urusi imesema iko tayari kukabidhi miili mingine 2,239 ya wanajeshi wa Ukraine, nje ya makubaliano ya awali.

Hii inaifanya kuwa maafikiano makubwa zaidi tangu uvamizi wa Urusi nchini Ukraine kuanza mwaka 2022.

Wakati huo huo, wasiopungua 59 wameuawa katika Ukanda wa Gaza kwa mashambulio mbalimbali.

Watu 30 waliuawa wakati vifaru vya Israel viliposhambulia umati wa watu waliokuwa wakijaribu kupata msaada kutoka kwenye malori.

Mashahidi waliohojiwa na shirika la habari la Reuters, walisema vifaru vya Israel vilifyatua makombora mawili kwenye umati wa watu waliokuwa wamekusanyika kwenye barabara kuu ya mashariki kupitia Khan Younis kwa matumaini ya kupata chakula kutoka kwenye malori ya misaada yanayotumia barabara hiyo.

Tukio hilo ni la karibuni zaidi katika mauaji ya karibu kila siku ya Wapalestina wanaotafuta msaada, katika muda wa wiki tatu tangu Israel iondoe vizuizi katika sehemu za kupitisha misaada ambavyo vimekuwapo kwa karibu miezi mitatu.

Israel imeruhusu misaada kuingia Gaza kupitia shirika jipya linaloungwa mkono na Amerika na Israel, ambalo linafanya usambazaji katika maeneo machache yanayolindwa na vikosi vyake.

Madaktari walisema mashambulio tofauti ya anga iliyolenga kambi ya wakimbizi ya Maghazi na kitongoji cha Zeitoun katikati na kaskazini mwa Gaza yaliwauwa watu wasiopungua 14, huku wengine watano wakiuawa katika shambulio la anga kwenye kambi ya hema huko Khan Younis kusini mwa Gaza.

Wengine 11 waliuawa katika shambulio la lililotekelezwa na Israeli dhidi ya umati wa Wapalestina waliokimbia makazi yao waliokuwa wakisubiri lori za misaada zilizoletwa na Umoja wa Mataifa kwenye barabara ya Salahuddin katikati mwa Gaza.

Jeshi la Ulinzi la Israel (IDF) lilisema linachunguza vifo vilivyoripotiwa vya watu waliokuwa wakisubiri chakula.

Siku ya Jumanne, wizara ya afya ya Gaza ilisema Wapalestina 397 kati ya wale wanaojaribu kupata msaada wa chakula wameuawa na zaidi ya 3,000 kujeruhiwa tangu mchakato wa kusambaza misaada kuruhusiwa tena mwishoni mwa Mei.