Kimataifa

Wabunge wa Amerika wagawanyika kuhusu mashambulizi Iran

Na REUTERS June 24th, 2025 Kusoma ni dakika: 2

WASHINGTON, Amerika

BAADHI ya wabunge wa vyama vya Democrats na Republican wamelitaka bunge la Congress kupitisha uamuzi wa kuzuia Amerika kuingilia mapigano yanayoendelea katika Mashariki ya Kati.

Lakini huenda uamuzi huo usipitishwe kwani viongozi wa Republican katika Seneti na Bunge la Wawakilishi wanaunga mkono hatua ya Amerika kushambulia vituo vya kinyuklia nchini Iran.

Seneta wa Virginia Tim Kaine (wa chama cha Democratic), alisema anatarajia kulazimisha Seneti kupiga kura wiki hii kwa hoja yake inayomtaka Rais Donald Trump kusitisha mashambulio dhidi ya Iran.

Kulingana seneta huyo, Amerika inafaa kupata idhini kutoka kwa Congress kwanza kabla ya kutekeleza mashambulio nchini Iran.

Katika Bunge la Wawakilishi, Thomas Massie wa Kentucky (Republican) na Ro Khanna wa California (Democratic) walisema wangetaka hoja kama hiyo waliyoiwasilisha katika bunge hilo ipigiwe kura.

“Amerika inaingia katika vita, kutokana na uamuzi wa Donald Trump, wala sio msukumo wa kulinda masilahi ya kitaifa ya Amerika, haswa bila suala hilo kujadiliwa na kupitishwa katika bunge la Congress,” Kaine akaambia shirika la habari la CBS kupitia kipindi “Face the Nation”.

Ikulu ya White House haikutoa kauli yoyote kuhusu kukosolewa kwa Trump na wabunge hao.

Hata hivyo, duru zinasema kuwa Spika wa Seneti Mike Johnson na Kiongozi wa Wengi katika John Thune walijulishwa mapema kuhusu shambulio la Amerika nchini Iran.

Wanachama wa bunge la Congress wanatarajiwa kupata maelezo kuhusu suala hilo Jumanne.

Afisi ya Thune ilikataa kutoa kauli yoyote kuhusu pendekezo la Kaine.

Shambulio la Amerika dhidi ya vituo vya kinyuklia vya Irani Jumamosi liliwagawanya viongozi wafuasi wa Trump, wengine wakimuunga mkono rais huku wengine wakiitaka Amerika isitishe mashambulio.

“Nawakilisha muungano ambao ulimchagua Rais Trump. Tulichoshwa na vita vya kila mara,” Massie akaambia CBS.

“Tuliahidi kuwa tutatoa kipaumbele kwa masilahi ya mashujaa wetu, tutanyoosha sera zetu za uhamiaji na kukarabati miundo msingi yetu.”

Mashambulio ya Amerika yalilenga vituo mahsusi vya mpagno wa kinyuklia nchini Iran.

Massie na Kaine walisema hakukuwa na dharura iliyomhitaji rais Trump kuchukua hatua kivyake.

“Hakukuwa na tishio kwa Amerika,” Massei alisema.

Ripoti kijasusi na wachanganuzi wanayo misimamo tofauti kuhusu jinsi Iran inajenga bomu ya nyuklia.

Mnamo Ijumaa Mkurugenzi wa Idara ya Kitaifa ya Ujasusi Tulsi Gabbard alisema kuwa Amerika ilipata habari kwamba endapo Iran itafanya hivyo, huenda ikaunda silaha za nyuklia ndani ya wiki au miezi michache.

Lakini maafisa wa Amerika wanasema hawaamini kuwa Iran ilikuwa ameamua kutengeza bomu.

Kwa upande wake Iran inadai mpango wake wa nyuklia haulengi vita bali unalenga kuzalishaji wa kawi na kuendesha utafiti wa kimatibabu.

Lakini mpango wake, ulioanza mwishoni mwa miaka ya 1950s kwa usaidizi wa Amerika, umegubikwa kwenye shauku katika miaka ya hivi karibuni.