Jamvi La Siasa

Fumbo la ‘mgeni anayesumbua’ ODM

Na RUSHDIE OUDIA February 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MFANYABIASHARA maarufu na anayejitambulisha kama “mwana wa kuasili” wa aliyekuwa Waziri Mkuu Raila Odinga, Bw Oketch Salah, anaendelea kukabiliwa na upinzani na kukataliwa na watu waliokuwa karibu na kiongozi huyo wa upinzani, kufuatia shughuli zake tata ndani ya chama cha Orange Democratic Movement (ODM).

Licha ya kuonekana mara kwa mara karibu na Odinga hata katika siku zake za mwisho, utata kuhusu Bw Salah na nafasi yake halisi ndani ya familia ya Odinga na siasa za ODM bado ni fumbo kubwa, hasa anapojaribu kujijenga katika mazingira ya kisiasa yanayobadilika ndani ya chama hicho cha zaidi ya miaka 20.

Odinga alipokuwa hai, aliwahi kumtambulisha Bw Salah katika mikutano kadhaa, lakini watu wa karibu na aliyekuwa Waziri Mkuu wanasema hawakuwahi kuelewa vyema jukumu lake wala kuwa na uhusiano wa karibu naye kibinafsi.

Ndani ya familia ya Jaramogi, kuna mitazamo tofauti kuhusu Bw Salah. Baadhi ya wanafamilia akiwemo Seneta wa Siaya Dkt Oburu Oginga, mwanawe Jaoko Oburu na Bi Ida Odinga wamewahi kumtambua katika majukwaa mbalimbali.

Hata hivyo, Winnie Odinga na Raila Odinga Jnr wamekana kumfahamu, wakipuuza madai yake kuhusu kuwa naye katika nyakati za mwisho za maisha ya Odinga.

Katika mahojiano hivi majuzi, Winnie alisema aliwahi kukutana na Bw Salah lakini akasisitiza kuwa hakuna anayemfahamu vyema, hata kupendekeza kuwa huenda ana matatizo ya kiakili au anafaa kuchunguzwa na Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI).

Mwanachama huyo wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) alikanusha vikali madai kuwa mfanyabiashara huyo alikuwa karibu na babake wakati wa ugonjwa wake wa mwisho, akitaja madai hayo kama “uwongo hatari” na kuhoji nia yake.

Kauli hizo zilijiri siku chache baada ya Bw Salah kudai hadharani kuwa alikuwa pamoja na Odinga tangu mwanzo wa ugonjwa wake hadi alipofariki, akisisitiza kuwa hakutoa taarifa hizo kwa nia ya kutafuta huruma au faida ya kisiasa bali kwa sababu ni ukweli.

Hata hivyo, ni kushiriki kwake katika masuala ya ODM kulikoibua dhoruba kubwa zaidi ndani ya chama, na kulazimisha uongozi wa juu kuingilia kati.

Bw Salah amehusishwa na mrengo wa ODM unaomuunga mkono kiongozi wa chama Dkt Oburu Oginga na pia kuunga mkono azma ya Rais William Ruto kutetea kiti chake mwaka 2027.

Ameandaa mikutano odm

Ameandaa mikutano mbalimbali ya chama na wafuasi pamoja na wajumbe kote nchini, akisema lengo lake ni kukipa umaarufu na kuimarisha ODM.

Hata hivyo, hatua hizo zimeanza kukosolewa vikali, huku Mwenyekiti wa ODM Bi Gladys Wanga akiwa wa hivi karibuni kujitokeza.

Bi Wanga alifafanua kuwa shughuli, kauli au mikutano inayofanywa na Bw Salah ni ya kibinafsi na haiwakilishi wala kuifunga ODM kwa namna yoyote.

Alisisitiza kuwa shughuli zote rasmi za ODM hupangwa na kuendeshwa kupitia afisi ya chama kwa idhini na mwongozo wa uongozi unaotolewa na Dkt Oburu Oginga.

Aliwaonya viongozi wa mashinani, wanachama na wafuasi kuwa hakuna shughuli yoyote inayopaswa kufanyika kwa jina la ODM bila mashauriano na idhini ya uongozi wa chama.

Aliongeza kuwa ODM itaendelea kudumisha nidhamu, utaratibu na ushirikishaji unaolenga kufikia malengo yake.

Kauli ya Bi Wanga ilitolewa siku moja baada ya Bw Salah kuandaa mkutano na wanafunzi wa vyuo vikuu katika Ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Kenyatta (KICC), uliogeuka vurugu na kumlazimu kuondoka kwa haraka.

Baada ya kuondoka, wanafunzi waliokuwa wamekusanyika chini ya kaulimbiu ya “Linda Comrade” walimkosoa vikali, wakaanza kusifu Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, wakimdhalilisha Bw Salah na kumuunga mkono mbunge huyo mwenye ushawishi mkubwa.

Katika kujitetea, Bw Salah alisema nia yake ni njema na anachotaka ni kuona ODM ikiwa na nguvu.

Alisema kila anachofanya ni kwa lengo moja tu la kukipa chama umaarufu na kukiimarisha, na akaomba radhi kwa Bi Wanga iwapo alimuudhi bila kukusudia.

Alisisitiza kuwa ODM inahitaji kupewa nguvu mpya na kufufuliwa, akiongeza kuwa harakati lazima ziendelee kuwafikia watu mashinani.

Mfanyabiashara huyo alisema kujitolea kwake kwa ODM si kwa kujionyesha bali ni kutimiza ahadi aliyompa aliyekuwa kiongozi wa chama, kwa kutumia rasilmali zake binafsi.

Mikutano ya Bw Salah kote nchini imeibua pia maswali kuhusu ufadhili wa shughuli za ODM zinazojulikana kama ‘Linda Ground’.

Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna na Mwakilishi wa Wanawake wa Kisumu Ruth Odinga wamedai kuwa fedha hizo zinatoka serikalini, ambayo inadaiwa kutaka kukidhibiti chama hicho kutoka Ikulu.

Bi Odinga alihoji nia ya mfadhili huyo, akisema kuwa malengo yake si mema, hasa ikizingatiwa gharama kubwa za helikopta, mahema makubwa na jezi zenye nembo ya ODM, ilhali chama kimekiri hadharani kuwa hakijatumia hata senti moja katika shughuli hizo.