Mhandisi ageuza eneo kame kuwa uga wa kilimo-mseto
UNAPOZURU eneo la Tala, Kaunti ya Machakos, haswa wakati huu sehemu nyingi za taifa zinashuhudia kiangazi na ukame, utakaribishwa na udongo na mimea iliyonyauka.
Inaomba angaa tone la maji ili kufufua hadhi ya ardhi.
Ni eneo ambalo wengi hulitazama kama kame, gumu na lisilotabirika kwa kilimo chenye manufaa, hasa wakati huu wa misukosuko ya mabadiliko ya tabianchi.
Kwa miongo mingi, Tala imetambulika kuwa miongoni mwa maeneo kame na nusu-kame (ASAL), hali inayoshuhudiwa zaidi kwa wafugaji wa kuhamahama.

Lakini katika kijiji cha Kwa Matingi, Matungulu, taswira hiyo ni tofauti. Historia imeandikwa upya. Mistari iliyopangwa vizuri ya vitunguu na nyanya, inaeleza simulizi tofauti.
Mifereji mieusi ya umwagiliaji maji kwenye mimea na mashamba, inastawisha vitunguu na nyanya. Hapa, mafanikio si ya kubahatisha ambayo yameletwa na teknolojia na mifumo ya unyunyiziaji mimea na mashamba maji.
Anayeongoza mageuzi hayo si mwingine, ila ni Suleiman Maundu Ramadhan, mhandisi kwa taaluma na mkulima hodari. Akitumia fikra za kihandisi zinazopigwa jeki na uvumilivu na imani, amegeuza shamba lake kuwa uga wa uzalishaji mazao mfululizo.

Maundu ni mwasisi wa kampuni ya uhandisi ya Ramtek Services Ltd, na amesomea kozi ya uhandisi wa mitambo, akifanya kazi na viwanda vya kuunda vileo na maji.
Pia, amenoa makali ya taaluma yake nchini Ujerumani. “Uhandisi ulinifundisha nidhamu, kupanga na kuzingatia kila hatua ya jambo. Kilimo kinahitaji mambo yayo hayo,” anaambia Akilimali.
Mwaka 2020, janga la Covid-19 lilipotua nchini, sekta na shughuli nyingi ziliathirika. Maundu alikuwa miongoni mwa walioathirika, haswa kutokana na amri ya ama kuingia au kutoka Kaunti ya Nairobi, na kaunti jirani.

Kujiendeleza kimaisha na kuhakikisha familia yake inapata riziki, aligeukia ekari 10 za shamba analomiliki Tala kushiriki kilimo.
Hapo ndipo Rama Farm Supplies Ltd ilipozaliwa. “Nilichagua vitunguu na nyanya, mazao yaliyokuwa na bei nzuri sokoni,” anaelezea.
Alianza kwa umakinifu, akilima ekari ekari nne za vitunguu na tatu za nyanya, huku mahindi na maharagwe yakitumika kuboresha udongo kwa njia ya mzunguko wa mimea.
Changamoto kubwa ilikuwa maji. “Eneo kame, kilimo cha kutegemea mvua hakiwezi kudumu,” anasema.
Maundu, kwenye mahojiano na Akilimali alifichua kwamba aliwekeza zaidi ya Sh2.5 milioni kwenye mifumo ya umwagiliaji mimea na mashamba maji kwa mifereji, maarufu kwa Kiingereza kama Irrigation.

Licha ya mahesabu hayo, vitunguu, anasema alikuwa ametabiria huenda kila kilo msimu wa mavuno ikampa zaidi ya Sh150 lakini akapigwa dafrau.
“Hata hivyo, kwa sababu ya amri ya watu kuzuiwa kuingia Nairobi na kaunti jirani, mambo yaligeuka. Bei nayo, hususan ya vitunguu ilinionyesha vimulimuli,” anakumbuka.
Kilo ya vitunguu vya mviringo anavyolima ilishuka hadi chini ya Sh50.
“Isitoshe, mazao mengi yaliozea kwenye maghala tukisubiri angaa bei iimarike,” anadokeza. Changamoto hiyo kando na kuchangiwa na virusi vya corona, wengi wa walioathirika waliingilia kilimo hivyo mazao yakawa mengi na kuathiri bei.

Jaribio la pili, mkulima mjasiriamali huyu anasema halikuwa baya ila bado alikadiria hasara. Hatimaye, la tatu na kuendelea, lilimkubali.
Leo hii, zaidi ya ekari 30 ziko chini ya mfumo wa umwagiliaji mimea na mashamba maji kwa mifereji, zikihudumiwa na mabwawa mawili na pampu za umeme na sola – zinazopampu hadi lita 600,000 za maji kwa siku.
Plum Agri Irrigation, kampuni ya Kenya inayotoa huduma za mifumo ya irrigation na uuzaji wa pembejeo za kilimo, imekuwa na mchango mkubwa kufanikisha azma ya Maundu.
“Umwagiliaji mimea na mashamba maji kwa kutumia mifereji ndio siri ya kukabiliana na uhaba wa chakula na njaa,” anasema Joshua Musyoka, meneja wa tawi la kampuni hiyo.

“Hata hivyo, lazima ufanywe kwa kutumia mifumo bora, iliyowekwa kwa usahihi baada ya tathmini ya kina ya eneo linalolengwa.”
Miaka mitano baadaye, Rama Farm ina zaidi ya ekari 40 zinazotumika kuzalisha chakula.
Vitunguu na nyanya ndizo nguzo kuu, zikizalishwa kwa mpangilio unaohakikisha uwepo wa mavuno kila mwezi. Vitunguu huzalisha tani 15–20 kwa ekari, huku nyanya tani 30–50.
Karibu asilimia 80 ya mazao huuza ndani ya nchi, huku asilimia 20 ikienda Uganda na Tanzania. Mradi wa Maundu umeajiri wafanyakazi 24 wa kudumu, na huandika makumi ya vibarua wakati wa mavuno.
