Amerika yaungana na Israeli kuishambulia Iran
AMERIKA na Israeli, Jumamosi zilizindua mashambulio makubwa ya kijeshi nchini Iran katika kile zinazotaja kama hatua ya “kukabiliana na tishio” kutoka Tehran.
Operesheni hiyo imebandikwa jina la Operation Lion’s Roar na ilianza kwa mfululizo wa mashambulizi yaliyolenga miji mikuu na vituo vya kijeshi Iran, ikiwemo Tehran, Isfahan, Qom na maeneo mengine.
Kwa mujibu wa taarifa za Wizara ya Ulinzi ya Israeli, shambulio hilo lilikuwa la kuzuia hatari kabla haijakuwa mbaya zaidi na lilipangwa kwa kushirikiana kwa karibu na Amerika kwa muda wa wiki kadhaa.
Israeli ilitangaza hali ya dharura katika nchi nzima baada ya mlipuko na mapigano kuanza Iran ikisema ilitingua makombora yaliyoelekezwa nchini humo na Iran.
Rais wa Amerika, Donald Trump, alithibitisha kushirikiana na Israeli kuanza “operesheni kubwa la kivita” dhidi ya Iran, akisisitiza kuwa lengo ni kuharibu uwezo wa kijeshi na kuzuia Iran kupata silaha za nyuklia.
Aliongeza kuwa hatua hii ni ya kutetea usalama wa Amerika na washirika wake.
“Tulijaribu mara kwa mara kufikia makubaliano ila hakuna lililotendeka,” alisema akiongeza kuwa nchi yake itaharibu makombora yao na kubomoa kabisa tasnia yao ya makombora.
Mashambulizi hayo yaliyofanyika sambamba na udukuzi wa tovuti za mashirika ya serikali ya Iran yalijiri licha ya mazungumzo ya kila mara ya kujaribu kuafikiana kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran.
Mashirika kadhaa ya habari yanayohusishwa na serikali ya Iran yameripotiwa kulengwa na mashambulizi ya kimtandao kufuatia mashambulizi ya kijeshi ya Amerika na Israeli dhidi ya Iran, kwa mujibu wa taarifa iliyochapishwa kwenye mtandao wa Telegram wa gazeti lenye msimamo mkali la Hamshahri.
Ripoti hiyo ilisema kuwa “wimbi kubwa” la operesheni za kimtandao lilianza sambamba na kuongezeka kwa mashambulizi ya kijeshi, huku majukwaa kadhaa makubwa ya habari ya ndani yakikumbwa na hitilafu au matatizo ya kiutendaji.
Kwa mujibu wa taarifa za awali zilizonukuliwa na kituo hicho, tovuti za Shirika la Habari la Serikali la IRNA na shirika la nusu-rasmi la ISNA zilikuwa miongoni mwa vyombo vilivyoripotiwa kudukuliwa.
Aidha, kulikuwa na taarifa za hitilafu zilizoathiri baadhi ya apu zinazotumika sana nchini Iran, ingawa maelezo zaidi kuhusu chanzo au aina ya mashambulizi hayo hayakuwa yamebainika mara moja.
Wiki chache kabla ya mashambulizi, Amerika na Iran zilikuwa zikifanya mazungumzo yaliyotarajiwa kuzaa matunda, lakini tofauti kuhusu kiwango cha mpango wa makombora ya Iran kilifanya yashindikane.
Vyombo vya habari vya Iran viliripoti milipuko ikiwemo katika mji mkuu Tehran.
Shirika la habari la serikali ya Iran lilithibitisha kwamba Rais wao Masoud Pezeshkian yuko salama, na Kiongozi Mkuu Ayatollah Ali.
Khamenei alihamishiwa katika eneo salama kutokana na hatari ya mashambulizi.
Serikali ya Israel ilifunga anga yake na kutangaza tahadhari kuhusu uwezekano wa mashambulizi ya kisasi kutoka Iran.
Hali hiyo ilisababisha Israel kutangaza hali ya dharura na kusimamisha safari za ndege za raia ili kupunguza hatari kwa wananchi.
Ingawa Iran imekuwa ikitetea nia yake ya kupata silaha za nyuklia, Amerika na washirika wake Ulaya wanadai kuwa juhudi hizo ni tishio kwa usalama wa kimataifa.