Habari

Wito Wakenya waondoke haraka Mashariki ya Kati

Na NDUBI MOTURI March 7th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

SERIKALI ya Kenya imewahimiza raia wake wanaoishi katika eneo la Mashariki ya Kati kuondoka haraka iwezekanavyo kwa kutumia ndege za kibiashara au za safari kuwarejesha nyumbani kwa gharama zao wenyewe.
Serikali pia imethibitisha kuwa hakuna Mkenya aliyeripotiwa kufariki au kujeruhiwa tangu mapigano kuanza wiki moja iliyopita.
Wito huo ulitolewa na Mkuu wa Mawaziri na Waziri wa Masuala ya Kigeni Musalia Mudavadi, ambaye alisema serikali inaendelea kufuatilia kwa karibu hali ya usalama katika eneo hilo huku ikiratibu juhudi za balozi zake kulinda raia wa Kenya walioko huko.
Katika taarifa iliyotolewa Ijumaa, Mudavadi alisema Wakenya wanaotaka kuondoka wanapaswa kupanga safari zao kupitia mashirika ya ndege ya kibiashara au maajenti wa usafiri walioidhinishwa, mradi hali ya usalama inaruhusu.
“Tunahimiza raia wa Kenya wanaotaka kuondoka katika eneo hilo kufanya mipango ya safari kupitia mashirika ya ndege yaliyopo au maajenti wa usafiri wanaotambulika,” alisema.
Kwa mujibu wa wizara, usalama na ustawi wa Wakenya wanaoishi nje ya nchi unasalia kuwa kipaumbele kikuu cha serikali. Wizara hiyo ilisema kuwa licha ya mvutano unaoendelea, Wakenya wengi katika eneo hilo bado wanaendelea na shughuli zao za kila siku kulingana na hali ya usalama katika maeneo wanayoishi.
Inakadiriwa kuwa zaidi ya Wakenya 500,000 wanaishi katika nchi mbalimbali za Mashariki ya Kati, wengi wao wakifanya kazi katika sekta za nyumbani, ujenzi, hoteli na huduma za afya.
Serikali pia imesema inaratibu juhudi za kuwasaidia wanaotaka kurejea nyumbani kupitia njia za kidiplomasia na usafiri wa anga. Shirika la ndege la taifa, Kenya Airways, tayari limeanza kutumia njia salama za anga zilizokubaliwa kusaidia kuwarejesha Wakenya waliokwama katika eneo hilo kadri hali ya usafiri wa anga inavyoathiriwa na mzozo unaoendelea.
Mudavadi alieleza kuwa wizara yake inaendelea kuwasiliana mara kwa mara na balozi za Kenya katika eneo la Mashariki ya Kati, ambazo kwa sasa zinajumuisha balozi saba pamoja na balozi ndogo mbili.
Balozi hizo zimeanzisha mifumo ya dharura na mipango ya kuwahamisha Wakenya iwapo hali ya usalama itadorora zaidi. Aidha, raia wa Kenya wanaoishi katika eneo hilo wamehimizwa kujisajili katika balozi au balozi ndogo za Kenya zilizo karibu nao ili iwe rahisi kupokea msaada au taarifa za dharura.
Serikali pia imeanzisha kituo cha saa 24 cha kusaidia Wakenya wanaoishi ughaibuni kupitia simu na WhatsApp. Kituo hicho kinatarajiwa kusaidia kutoa mwongozo, kusaidia Wakenya wanaokumbwa na matatizo na kuwaunganisha na balozi za Kenya katika eneo hilo.
Mashariki ya Kati ni mojawapo ya maeneo muhimu kwa ajira za Wakenya wanaoishi ughaibuni. Fedha wanazotuma nyumbani ni chanzo kikubwa cha fedha za kigeni kwa Kenya.
Aidha, eneo hilo ni soko muhimu kwa bidhaa za Kenya, hasa mazao ya kilimo kama maua, matunda na mboga. Kufikia mwaka 2024, biashara kati ya Kenya na nchi za Ghuba kama United Arab Emirates, Saudi Arabia na Qatar ilifikia takriban dola bilioni sita.
Hata hivyo, Wizara ya Masuala ya Kigeni imeonya kuwa mzozo unaoendelea unaweza kuvuruga biashara, hasa usafirishaji wa bidhaa zinazoharibika haraka ambazo hutegemea sana usafiri wa anga kuelekea masoko ya Ghuba. Serikali imesema inaendelea kushirikiana na mashirika ya ndege kuhakikisha mauzo ya nje yanaendelea licha ya changamoto za safari za anga.