Sifuna: Wanadai kuzima vuguvugu letu la ‘Linda Mwananchi’
JUHUDI za kuzima vuguvugu la Linda Mwananchi zinaendelea kufichuka huku likiendelea kufanya mikutano ya kisiasa nchini.
Kiongozi wa kundi hilo na Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna anadai kuwa kuna juhudi za makusudi za kuzima shughuli zao, kuanzia kuvurugwa kwa mikutano yao, madai ya kujaribiwa kununuliwa kwa fedha nyingi hadi kuzuiwa kwa mipango ya kidijitali ya kuratibu shughuli zao.
Akizungumza katika mkutano wa People’s Dialogue Festival uliofanyika Uhuru Park, Sifuna alisema kundi lake limekumbana na vikwazo mara kadhaa tangu lianze mikutano ya Linda Mwananchi kote nchini.
“Tunafahamu kuna propaganda eti tuliitisha hadi Sh2 bilioni ili tusitishe kampeni yetu. Lakini vuguvugu hili ni kubwa kuliko mtu mmoja, hatutakubali kununuliwa,” alisema Sifuna.
Mikutano yao ya kisiasa imekumbwa na vurugu au vizingiti vinavyodaiwa kulenga kupunguza ushawishi wao.
Seneta wa Siaya James Orengo, ambaye pia amehusishwa na msimamo mkali wa kuikosoa serikali ya sasa, amewahi kuonya kuhusu kile alichokiita juhudi za kuzuia maoni tofauti katika siasa za Kenya.
Orengo amesisitiza mara kadhaa kuwa demokrasia haiwezi kustawi ikiwa makundi ya kisiasa yatazuiwa kuwasilisha maoni yao hadharani. “Katika demokrasia, lazima kuwe na nafasi ya sauti tofauti kusikika bila vitisho au vikwazo,” amewahi kusema katika mikutano ya kisiasa na mahojiano ya vyombo vya habari.
Mbali na kuvurugwa kwa mikutano, viongozi wa Linda Mwananchi pia wanadai kuwa kuna juhudi za kuwapa baadhi yao pesa ili waachane na vuguvugu hilo.
Sifuna alisema propaganda pia zimesambazwa zikidai kuwa aliomba pesa ili aachane na kampeni dhidi ya serikali jumuishi.
“Walianza kueneza propaganda kwamba nimeomba pesa ili kuacha vuguvugu hili. Ukweli ni kwamba sisi hatutayumbishwa na fedha,” alisema.
Kundi hilo pia linadai kuwa juhudi zao za kuanzisha tovuti na nambari ya kuchangisha pesa kutoka kwa wafuasi zimekuwa zikitatizwa mara kadhaa.
Kwa mujibu wa Sifuna, wafuasi wao walitaka kutumia mifumo ya kidijitali kuratibu mikutano na michango ya kuendesha kampeni za Linda Mwananchi, lakini mipango hiyo imekuwa ikizuiwa.
“Tumekuwa tukijaribu kuanzisha tovuti na nambari ya kuchangisha fedha lakini kila mara tunakumbana na vikwazo,” alisema.
Katika hatua nyingine iliyoibua utata, viongozi wa kundi hilo wanapinga jaribio la kusajili chama kipya kiitwacho Linda Mwananchi Party.”
Kupitia mawakili wao, Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino waliwasilisha malalamishi kwa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Kisiasa wakisema hawahusiki na juhudi hizo.
Walionya kuwa kusajili chama hicho kunaweza kuwapotosha wafuasi na hata kutumiwa vibaya kukusanya fedha kwa jina la vuguvugu lao.
Kulingana na mchanganuzi wa siasa Dkt Isaac Gichuki, mpango wa kusajili jina la vuguguvu hilo kama chama ni mkakati wa kulizima.
Anasema hatua ya ODM kumvua Sifuna wadhifa wake wa Katibu Mkuu ni sehemu ya mkakati wa kuzima ushawishi wa Linda Mwananchi unaoendelea kuongezeka.
Ingawa uamuzi huo ulizuiwa na mahakama kwa muda, wafuasi wa Linda Mwananchi wanadai kuwa hatua hiyo ilikuwa sehemu ya mkakati mpana wa kudhoofisha vuguvugu lao ndani ya chama.
Mvutano huo unajiri wakati ODM inakabiliwa na mgawanyiko wa ndani kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027 huku makundi mawili makuu –Linda Mwananchi linalokosoa ushirikiano wa kisiasa na serikali, na Linda Ground linalounga mkono ushirikiano huo yakikosoana.
Chama hicho kinatarajiwa kufanya mkutano wa wajumbe baadaye mwezi huu ambao dalili zinaashiria utaendeleza mgawanyiko baada ya wafuasi wa Linda Mwananchi kupinga ajenda zilizowekwa.
Wadadisi wa siasa wanasema kuvurugwa kwa mikutano ya Linda Mwananchi na maafisa wa usalama huku ile ya Linda Ground inayoongozwa na kiongozi wa ODM Oburu Odinga ikifanyika kwa amani ni ishara ya mkakati mpana wa kuzima vuguvugu hilo.
Huku mvutano ukizidi, wachambuzi wa siasa wanasema mbinu zinazodaiwa kutumika kuzima Linda Mwananchi zinaendelea kujenga kundi hilo linaloungwa mkono na vijana ambao ndio wengi nchini.
“Ni wazi kuwa kila uchao kuna njama zinazosukwa kuzima Linda Mwananchi ikiwemo madai ya mbunge mmoja kuhusisha jina hilo na kauli au shughuli za kijeshi. Wasichojua wanaofanya hivyo ni kuwa wanaendelea kulijenga jina hilo. Vuguvugu linaloanzishwa na watu huwa na nguvu zinazoweza kushinda muungano wa tabaka la wanasiasa wenye ushawishi,” akasema mchambuzi wa siasa Diana Avisa.