Kimataifa

Vita vyachacha Trump akiitaka Iran ijisalimishe

March 8th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

VITA kati ya Iran na Amerika vimeingia wiki ya pili huku hofu ikiongezeka kwamba huenda mapigano hayo yakakosa kufikia mwisho hivi karibuni.

Mashambulizi ya pande zote yameendelea kuripotiwa katika maeneo mbalimbali Mashariki ya Kati, huku juhudi za kidiplomasia zikionekana kukosa kuzaa matunda.

Rais wa Amerika, Donald Trump, alizua mjadala mkali baada ya kuitaka Tehran ijisalimishe “bila masharti.”

Kupitia ujumbe aliochapisha katika jukwaa lake la Truth Social, Trump alisema hakutakuwa na mazungumzo au makubaliano na Iran hadi serikali ya nchi hiyo itakapokubali masharti hayo.

Kauli hiyo ilitolewa saa chache baada ya Rais wa Iran Masoud Pezeshkian kudokeza katika mitandao ya kijamii kuwa baadhi ya mataifa yameanza juhudi za kusuluhisha mgogoro huo.

Kauli yake ilizua matumaini kwamba mazungumzo ya amani yanaweza kuanza, lakini matamshi ya Trump yalionekana kufifisha matumaini hayo.
Katika siku za hivi karibuni, mashambulizi ya makombora na ndege za kivita yameendelea kati ya Iran na Israel.

Jeshi la Israeli lilisema mifumo yake ya ulinzi wa anga ilifanikiwa kuzuia makombora kadhaa yaliyofyatuliwa kutoka Iran kuelekea maeneo ya Israel.

Milipuko ilisikika katika baadhi ya maeneo huku wanajeshi wakijaribu kudhibiti makombora hayo kabla ya kufika ardhini.

Baadaye, Israeli ilitangaza kuwa imeanzisha mashambulizi mapya dhidi ya miundombinu ya kijeshi katika mji mkuu wa Iran, Tehran.

Mashambulizi pia yaliripotiwa Lebanon, hasa katika mji mkuu Beirut, yakilenga maeneo yanayodaiwa kutumiwa na wanamgambo wa Hezbollah wanaoungwa mkono na Iran.

Kwa mujibu wa balozi wa Iran katika Umoja wa Mataifa, Amir Saeid Iravani, mashambulizi ya Amerika na Israeli yamesababisha vifo vya zaidi ya raia 1,300 nchini Iran huku maelfu wakijeruhiwa.

Kwa upande mwingine, mashambulizi ya Iran yameripotiwa kusababisha vifo vya watu kadhaa nchini Israeli pamoja na wanajeshi wa Amerika.
Mgogoro huo pia umewaathiri vibaya raia katika nchi jirani.

Nchini Lebanon, maelfu ya wakazi wamekimbia makazi yao baada ya mashambulizi makali ya anga katika vitongoji vya kusini mwa Beirut.

Shirika la misaada la Norwegian Refugee Council lilisema takriban watu 300,000 wamehamishwa ndani ya siku chache zilizopita.

Athari za vita hivyo zimeonekana pia katika uchumi wa dunia.

Masoko ya hisa barani Ulaya na Amerika yalishuka, huku bei ya mafuta ikipanda kwa kiwango kikubwa kutokana na hofu ya kuvurugika kwa usafirishaji wa mafuta kupitia Mkondo wa Hormuz, njia muhimu inayopitisha karibu theluthi moja ya mafuta yanayosafirishwa duniani.

Wakati huo huo, mvutano wa kisiasa umeongezeka baada ya Trump kusema Amerika inataka kushiriki katika mchakato wa kuchagua kiongozi mpya wa juu wa Iran.

Hata hivyo, Iran imekataa wazo hilo, ikisisitiza kuwa uamuzi huo utafanywa kulingana na katiba ya nchi hiyo na mapenzi ya wananchi wake pekee bila kuingiliwa na mataifa ya kigeni.