Kimataifa

Iran yateua Mojtaba kuwa Ayatollah mpya licha ya pingamizi za Trump

Na REUTERS March 9th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

DUBAI, UAE

UONGOZI wa kidini wa Iran umechagua makabiliano badala ya maridhiano na Amerika-Israel kwa kumteua Mojtaba Khamenei kuwa mrithi wa babake, Ali Khamenei.

Hatua hii inafasiriwa kama ukaidi dhidi ya Rais wa Amerika Donald Trump ambaye alikuwa ametangaza kuwa Mojtaba “hakubaliki”.

Kiongozi Mkuu wa Kidini wa Iran Ayatollah Ali Khamenei aliuawa katika shambulio lililotekelezwa na Amerika na Israel mwanzo mwa vita ambavyo sasa vimeingia wiki yake ya pili.

Hatua ya Baraza la Wataalamu kuteua Mojtaba kama mrithi wake imetoa nafasi kwa wenye msimamo mkali kusimamia Iran na hivyo kuashiria kuwa huenda vita kati yake na Amerika na Israel vikaenea nje ya ukanda wa Mashariki ya Kati.

“Kumpa Mojtaba nafasi ya kutwaa mamlaka ni kuendeleza mtindo wa zamani wa marehemu babake,” akasema Alex Vatanka, afisi mkuu katika tasisi ya Middle East Institute.

“Ni pigo kubwa kwa Amerika kuendesha operesheni ya kiwango hiki, kuchukua hatua kadhaa hatari, na kuishia kumuua mzee huyo mwenye umri wa miaka 86, kisha nafasi yake ipewe mwanawe mwenye msimamo mkali,” akaongeza.

Chini ya mfumo changamano wa uongozi nchini Iran, kiongozi mkuu wa kidini ndiye mwenye usemi na mamlaka makuu kuhusu masuala kama sera za kigeni na mpango wa nyuklia nchini humo. Kiongozi huyo pia hutoa mwongozo kwa Rais aliyechaguliwa pamoja na asasi ya bunge.

Wachanganuzi wanasema kuteuliwa kwa Mojtaba, kiongozi wa kidini mwenye msimamo kali na ambaye mkewe, mamake na watu wa familia yake pia waliuawa katika mashambulio ya Amerika na Israel kunatoa ujumbe wa wazi: Uongozi wa Iran umekataa kulegeza msimamo.

Imefanya hivyo ili kulinda na kudumisha mfumo na hauko tayari kufuata mkondo mwingine isipokuwa makabiliano, kulipisha kisasi na ustahamilifu.

Kulingana na wajuzi nchini Iran, Mojtaba hata hivyo atakumbwa na presha kutoka kwa raia wasioridhika na kuenea kwa vita, lakini anatarajiwa kuchukua hatua ya haraka kujikita kimamlaka.

Hiyo itamaanisha kupanua mamlaka ya Jeshi la Iran, kuweka sheria kali za kuongoza masuala ya ndani nchini humo na hatua kali kuchukuliwa dhidi ya waasi.

“Ulimwengu utakosa enzi ya utawala wa babake,” afisa mmoja wa ukanda huo mwenye uhusiano wa karibu na Iran aliambia Reuters.

“Mojtaba hatakuwa na chaguo lingine ila kudhihirisha uongozi wa kiimla……. hata kama vita vitaisha na atakabiliana vikali na wakosoaji wa serikali.

Hatua hiyo inajiri miezi kadhaa ya machafuko nchini Iran, mabaya zaidi kuwahi kushuhudiwa tangu Mapinduzi ya 1979.

Machafuko hayo yalikuwa yamedhoofisha Jamhuri hiyo ya Kiislamu hata kabla ya vita vya sasa kuanza.

Iran ilikuwa inakumbwa na changamoto za kusambaratika kwa uchumi, mfumko wa bei, kudorora kwa thamani ya sarafu yake na kuongezeka kwa umasikini.

Maandamano yalishuhudiwa katika miji kadhaa, raia wakionyesha hasira zao dhidi ya utawala dhalimu, hali ambayo huenda ikaendelea kushuhudiwa chini ya uongozi wa nyakati hizi za vita.