Kimataifa

Trump aambia Iran Ayatollah mpya Mojtaba hatadumu, kwamba ni ‘mwepesi’ kwake

Na REUTERS March 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

RAIS wa Amerika Donald Trump sasa anasema Amerika itamlenga Kiongozi mpya wa Kidini wa Iran Mojtaba Khamenei, mwanawe Kiongozi Mkuu Ali Khamenei aliyeuawa katika shambulio la Amerika-Israel mnamo Februari 28.  

Mojtaba, 56, ndiye Ayatollah mpya wa Iran, wadhifa ambao babake alishikilia tangu 1986. Uteuzi wake umemchemsha Trump huku Mojtaba, kama tu babake, akitarajiwa kulipiza kisasi na kuendeleza uhasama mkubwa dhidi ya Amerika.

Kauli ya Trump mnamo Jumapili kuwa lazima ahusishwe kwenye mchakato wa kumteua Kiongozi mpya wa Iran sasa ina maana kwamba Amerika italenga kuua Mojtaba ambaye mkewe, mwanawe na wanafamilia wake wengine wakiwemo babake na mamake washaangamizwa na Amerika.

“Kiongozi mpya Iran hatahudumu kwa kipindi kirefu iwapo atateuliwa bila idhini yetu, hatahudumu,” akasema Trump. Saa chache baada ya tamko la Trump, Iran nayo ilitangaza Mojtaba kama mrithi wa babake.

“Tunataka kuhakikisha kwamba haturudi nyuma kila baada ya miaka 10 mkiwa hamna rais kama mimi,” akaongeza.

Baada ya kuteuliwa kwa Mojtaba, Waziri wa Masuala ya Nje Abbas Araghchi alisema wapo tayari kushirikiana naye kwa ajili ya usalama na ulinzi wa Iran.

“Tuendelee kulinda haki za raia wa Iran na pia kuendeleza maslahi yao ya kitaifa na usalama. Hakuna hata muda kidogo ambao tutalegeza kamba kuhusu hili,” akasema Araghchi.

“Tutamheshimu kamanda mkuu hadi kwenye tone la mwisho la damu yetu,” akaongeza.

Hata hivyo, Trump amesisitiza kuwa hawezi kumkubali Mojtaba kwa sababu ataendeleza tu msimamo mgumu kama tu ya Ayatollah Khamenei.

Alisema Iran ‘inapoteza wakati wake’ kwa Mojtaba huku akisema kuwa mwana huyo wa pili wa kiume wa marehemu Ayatollah Khamenei ni ‘mwepesi’ kwake.