Habari Mseto

Ushahidi kuhusu kifo cha Prof Ken Walibora waanza kutolewa

Na RICHARD MUNGUTI March 10th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

CHOKORAA waliwapelekea polisi kitambulisho na ufunguo wa gari wa marehemu gwiji wa Kiswahili Prof Ken Walibora, Mkurugenzi wa Mawasiliano Wizara ya Utalii na Wanyamapori Hezekiel Gikambi aliambia Mahakama ya Milimani jana.

Huku akishindwa kuyazuia machozi kizimbani, Bw Gikambi alimweleza Hakimu Mwandamizi Paul Mutai kwamba alimsaka Prof Walibora kwa siku tano hadi alipompata katika chumba cha kuhifadhia maiti cha Hospitali ya Kenyatta (KNH) mnamo Aprili 15, 2020.

Bw Gikambi alisema alimsaka Prof Walibora katika Mochari ya City na hata katika vituo vya polisi bila ufanisi. Mkurugenzi huyo wa mawasiliano alisema alipashwa habari za maiti iliyokuwa KNH na Mkuu wa Kituo cha Polisi cha Kamkunji (OCPD) Mark Wanzala akielekea Kituo cha Polisi cha Muthangari kupiga ripoti ya mtu aliyepotea.

Bw Gikambi aliambia korti kuwa akiwa njiani kuelekea Muthangari alipokea simu ya Bw Wanzala akimtaka afike KNH kutambua mwili uliokuwa umehifadhiwa wa mwanaume Mwafrika asiyejulikana.

Mkurugenzi wa Mawasiliano Wizara ya Utalii na Wanyamapori Hezekiel Gikambi akitoa ushahidi kuhusiana na mauti ya mwandishi na mkereketwa maarufu wa Kiswahili, Prof Ken Walibora, jana. Picha|Richard Munguti

Bw Wanzala alimweleza Bw Gikambi atampata Inspekta Mukonambi Matumbufu na maafisa wengine wawili wa polisi.

Bw Gikambi, aliyekuwa afisa wa mawasiliano wa KNH kati ya 2018-2021, alimpigia simu meneja wa mochari ya KNH na kumsihi amuruhusu yeye (Gikambi na binamu wa Prof Walibora) watazame mwili huo.

“Mochari ilipofunguliwa na kuonyeshwa mwili, niliutambua kuwa wa Prof Walibora,” Bw Gikambi alisema huku amejaa huzuni.

Aliambia mahakama alikuwa pia ameandamana na nduguye marehemu Dk Arthur Wafula na watu wengine wa familia.

Mahakama iliambiwa kwamba makundi mbalimbali ya watu wakiwa wakuu wa Nation Media Group (NMG), Wahariri wa Gazeti la Taifa Leo wakiongozwa na Bw Stephen Musamali walikuwa wamaelezea hofu kuhusu usalama wa Prof Walibora baada ya mitandao ya kijamii kuchapisha habari alikuwa amehusika kwenye ajali.

Bw Gikambi alisema kabla ya kuelekezwa KNH na OCPD Matumbufu alikuwa ameenda katika makazi ya Prof Walibora mtaani Lavington na kuelezewa na mlinzi wa makazi yake kwamba “Prof Ken alitoka Aprili 10, 2020 saa moja asubuhi na hakurudi”.

“Nilipiga selfie kwa mlango uliokuwa umefungwa wa makazi ya Prof Walibora nikatuma kwa mitandao kadhaa ya Whatsapp iliyokuwa imeeleza wasiwasi kuhusu Prof Walibora kuthibitisha hayuko kwa makazi yake,” akasema Bw Gikambi.

Shahidi huyu alisema Prof Clara Momanyi wa Chuo Kikuu cha Katoliki cha Afrika Masharika (CUEA) – alikuwa akimsaka pamoja Bw Musamali wa Taifa Leo.

Chuo cha CUEA kilikuwa kimeanza mradi wa uandishi wa vitabu na kilikuwa kinataka mchango wake ilhali Taifa Leo ilikuwa ikisubiri Makala ya Jarida la Lugha na Fasihi.

Bw Gikambi alisema mwili wa Prof Walibora ulikuwa na majeraha kichwani na mkono wake ulikuwa umekatwa na kifaa chenye makali kama kisu.

Mahakama ilielezwa kwamba Prof Walibora aligongwa na matatu akiwatoroka wezi katika eneo la Muthurwa
Mahakama ya Milimani inachunguza kilichosababisha kifo cha Walibora.