Hivi vita lazima kuwe na mshindi, Iran yaambia Amerika na Israel
TEHRAN, IRAN
IRAN imesema wao ndio wataamua ni lini vita kati yao na Amerika-Israel vitaisha huku wakisisitiza kuwa hakuna mafuta yoyote yatakayosafirishwa nje ya Ukanda wa Mashariki ya Kati iwapo wataendelea kushambuliwa.
Rais Donald Trump alikuwa amenukuliwa akisema vita hivyo vitaisha ndani ya wiki nne au hata mapema zaidi kwa sababu Amerika imedhoofisha na kulemeza kabisa jeshi la Iran.
Hata hivyo, wanajeshi wa Iran wanasema lazima vita hivyo viwe na mshindi na bado wapo vitani na Amerika-Israel.
“Sisi ndio tutaamua ni lini vita vitaisha tena kwa njia gani kwa sababu lazima kuwe na mshindi. Kauli ya Trump ni upuzi tu,” ikasema taarifa ya jeshi la Iran iliyopeperushwa kwenye vyombo vya habari vya taifa hilo la Kiislamu.
Trump alikuwa ameonya kwamba iwapo Iran haitajisalimisha na kukoma kuzuia usafirishaji wa mafuta Mashariki ya Kati, basi watalengwa zaidi.
“Iwapo Iran itafanya chochote cha kuzuia usafirishaji wa mafuta ndani ya Strait of Hormuz, watapigwa na Amerika kwa uzito wa mara 20 zaidi kuliko hapo awali,” akasema Trump.
Strait of Hormuz ndiyo njia ya kusafirisha mafuta ambayo inaunganisha mataifa yanayozalisha bidhaa hiyo ya Gulf na Oman pamoja na Kisiwa cha Arabian. Huwa inahusika na humusi ya mafuta yanayosafirishwa ulimwenguni.
Kwa sasa Strait of Hormuz imefungwa na meli za kusafirisha mafuta hazipo safarini, hali ambayo huenda ikachangia kupanda kwa bei ya mafuta ghafi.
“Tutawashambulia kiasi kwamba itakuwa vigumu tena kwao kuamka au kufufua taifa lao hata kwa msaada wa washirika wao,” akaongeza Trump.
Iran mnamo Jumapili ilikaidi Amerika na kumtaja Mojtaba Khamenei kama kiongozi mpya wa kidini Amerika.
Israel nayo inasema kuwa vita vitaisha tu iwapo watauondoa utawala wa kiimla wa kiongozi wa kidini.
“Lengo letu ni kuhakikisha kuwa raia wa Iran wana sauti katika kumchagua kiongozi wao. Mwishowe ni wao ndio wataamua lakini tukifaulu pamoja na watu wa Iran basi tutamaliza kabisa uhasama na vita ambavyo vimekwepo kwa miaka mingi,” akasema Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu.
Maafisa wa Amerika wamekuwa wakisema lengo lao ni kuharibu kabisa nyuklia lakini Trump naye anasisitiza kwamba lazima waamue mustakabali wa uongozi wa Iran.
Tangu vita hivyo vianze mwisho wa Februari zaidi ya raia 1332 wa Iran wameuawa na wengi kujeruhiwa.
Waziri wa Masuala ya Nje wa Iran Abbas Araqchi alisema kuwa hawana nia ya kuendelea kuzungumza na Amerika na sasa wanamakinikia kushinda vita.
“Bado walituvamia wakati mazungumzo yalikuwa yamefikia hatua muhimu. Kuzungumza na Amerika si ajenda yetu tena, huko tumetoka,” akasema waziri huyo.