Ni jukumu letu sote kudhibiti mafuriko maeneo tunakoishi
JINSI wanavyosema vijijini kuwa kifo ni chako na mazishi ni yetu, nimeanza kusadiki hilo.
Kwamba unapofariki maiti yako wataamua watakayoifanyia watu wanaopumua, mahasidi watasema yao, rafiki zako watashuhudia ya kweli na uongo ila mara nyingi wanapenda kumpamba marehemu.
Tunatakiwa kujifunza hilo kutokana na mafuriko ya hivi majuzi ambayo yamesababisha vifo vya karibu watu 50.
Mafuriko hayo hayakuchagua nafasi wanayoshikilia watu katika nchi. Wote waliathirika.
Athari ya mvua katika jiji la Nairobi na viunga vyake ilitosha kushinda maradhi ya Covid 19.
Msiba ulikuwa mmoja vilio ndivyo vilivyokuwa tofauti. Mitaa ya mabanda ambayo hukabiliwa na mafuriko haikuwa tofauti na maeneo ya matajari kwa lugha yetu kijijini Soysambu katika kata ndogo ya Mawe – Tatu. Panaitwa hivyo, eneo bunge la Likuyani.
Haya turejee kwa mafuriko ya Nairobi.
Jinsi inavyosemwa siku unayokwenda uchi unakutana na mkweo. Mkwe wetu hapa alikuwa mvua iliyokuja kwa ghafla na dharura kubwa. Madereva magari yao yakazima kwa ghafla.
Watu wakaishi barabarani kwa muda mrefu mno, wengine wakalala mjini. Nyumbani kulikuwa hakuendeki, walikuwa huko hawakutaka kutoka.
Ngurumo za radi zilipiga kushinda parapanda ya siku ya kiama. Baadhi tulidhania ulimwengu umeisha.
Mizaha ikawa mingi, safari ya Singapore ikatajwa na watani kuwa Singapool.
Watu waliogelea barabarani kuokoa nafsi zao, baadhi wakaonja mauti. Ni msimu wa wingu kubwa la huzuni ambalo baadhi tumechangia. Mikondo ya kuelekezea maji taka imezibwa.
Kaunti ya Nairobi imelaumiwa kwa kutowajibikia mazingira ya jijini. Gavana Sakaja amejitetea kuwa atajaribu awezavyo kuhakikisha madhara sampuli hiyo hayatukii tena.
Kenya tunapenda kuishi katika nyumba za majaribio. Baadhi wamejenga katika maeneo yaliyokuwa chemichemi za maji. Wamenunua na kulipa na kuwatafuta masikini wapangaji wanaotafuta usingizi.
Wengi hawajapoteza tu huo usingizi hata mifumo ya maisha yao imevurugika.
Tuna wizara za mazingira na ardhi ambazo zina tabia ovyo.
Ikiwa kungekuwa na ufuatiliaji wa kanuni za ujenzi haya maafa hayangalitupata kama taifa. Sasa tupo hapo.
Huu ni wakati serikali inatakiwa kukabiliana na wale wanaokiuka kanuni za ujenzi. Majengo haramu yabomolewe, roho zingine zisipotee kiholela.
Tunataka wanaojenga shule wachukue tahadhari wanafunzi wao wasipotee kabla ya kufikia malengo yao ya kuwa watu wakubwa katika jamii katika siku zijao.
Wadau husika wawe na mpango endelevu wa kukabiliana na majanga hayo.
Lakini muhimu ni kuchukua tahadhari kabla ya hatari. Si wakati wa kubembelezana, Nairobi ndiyo makao makuu ya shirika la mazingira duniani. Katika kanda tunavuma, tujitazame.