Habari

Rais Ruto anatarajiwa kupeleka minofu Nyanza baada ya ziara yake ya Magharibi

Na RUSHDIE OUDIA na DOMNIC OMBOK March 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

BAADA ya kukamilisha ziara ya siku nne katika eneo la Magharibi, Rais William Ruto anatarajiwa kuanza mojawapo ya majukumu muhimu zaidi ya kisiasa ya kuwashawishi wakazi wa Nyanza kuunga mkono makubaliano ya kabla ya uchaguzi kati ya serikali yake na Orange Democratic Movement (ODM) kabla ya Uchaguzi Mkuu wa 2027.
Kwa mujibu wa ratiba ya awali, ziara ya Rais ya siku tano itaanza kwa mkutano muhimu na viongozi wa eneo hilo katika Ikulu Ndogo ya Kisumu Ijumaa alasiri.
Siku ya Jumamosi, Rais atazindua rasmi ujenzi wa reli ya kisasa kutoka Naivasha hadi Kisumu na Malaba saa tatu na nusu asubuhi, kabla ya kuzindua mradi wa nyumba za gharama nafuu katika eneo la Yala, Kaunti ya Siaya.
Rais wa Uganda Yoweri Museveni, ambaye pia ni mwenyekiti wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, anatarajiwa kuhudhuria hafla hiyo.
Baadaye, Rais ataelekea katika kituo cha uvuvi cha Asat katika Kaunti ya Kisumu na kukagua ujenzi wa barabara ya Holo–Lela katika eneo la Seme.
Jumapili, Rais Ruto atahudhuria ibada ya kanisa katika eneo la Sikri, Kaunti ya Homa Bay, kabla ya kuzindua miradi ya maendeleo katika maeneo ya Adiedo na Rusinga, kisha kurejea Chemelil katika Kaunti ya Kisumu kukagua miradi mingine saa kumi jioni.
Mnamo Jumatatu, Rais atakagua ujenzi wa daraja la Dho Goye katika eneo la Usenge, Bondo (Siaya), kabla ya kuelekea Bar Ober saa tano na nusu asubuhi na baadaye kusafiri hadi Sori katika Kaunti ya Migori.
Ratiba ya Jumanne bado haijawekwa wazi, lakini Rais anatarajiwa kuendelea na shughuli zake eneo la Nyanza ambalo kwa muda mrefu limekuwa ngome ya kisiasa ya aliyekuwa mpinzani wake na baadaye mshirika wake, Raila Odinga.
Wachambuzi wa siasa wanasema ziara hiyo ya siku tano katika eneo la Luo Nyanza ina uzito mkubwa wa kisiasa, ikitoa fursa kwa viongozi wa ODM wakiongozwa na Oburu Oginga kuwashawishi wafuasi wao kuwa makubaliano ya kabla ya uchaguzi na serikali yanaweza kuwa na manufaa.
Mkutano wa faragha kati ya Rais na viongozi wa Nyanza Ijumaa ulitarajiwa kuweka mwelekeo wa ziara hiyo. Baadaye, Rais pia alikutana na jamii ya Waislamu mjini Kisumu wakati wa maadhimisho ya Idd ul-Fitr.
Mchambuzi wa siasa Salim Odeny anaamini ziara hiyo itakuwa na mwelekeo wa kisiasa zaidi kuliko maendeleo.
“Rais anajaribu kujijenga moja kwa moja kwa wapiga kura katika eneo ambalo halijamuunga mkono kikamilifu. Pia anataka kutuma ujumbe kwamba anaunga mkono kikamilifu makubaliano ya kabla ya uchaguzi na ODM,” alisema Odeny.
Hata hivyo, juhudi za Rais zinafanyika wakati ambapo kundi lingine ndani ya ODM linaendesha kampeni ya kumpinga Rais kwa kaulimbiu ya Linda Mwananchi.
Mnamo Februari 11, 2026, Kamati Kuu ya ODM ilikutana Mombasa na kukubaliana kuimarisha ushirikiano na serikali ya Kenya Kwanza pamoja na kuidhinisha mazungumzo ya miungano mipya ya kabla ya uchaguzi.
Uamuzi huo unatarajiwa kuthibitishwa katika Mkutano Mkuu wa Wajumbe wa chama hicho utakaofanyika Machi 27.
Uzinduzi wa miradi ya maendeleo katika eneo ambalo kwa muda mrefu limekuwa likidai kutengwa kisiasa unaweza pia kumsaidia Rais kupata uungwaji mkono zaidi.
Miongoni mwa miradi mikubwa ni upanuzi wa reli ya SGR kutoka Naivasha hadi Kisumu na Malaba, mradi unaotarajiwa kuchochea ukuaji wa uchumi wa eneo hilo.
Gavana wa Kisumu Anyang’ Nyong’o alisema mradi huo utaleta mabadiliko makubwa kiuchumi na kuimarisha ushirikiano wa kikanda.
“Hatua hii si tu maendeleo ya miundombinu bali pia inaonyesha maono ya pamoja ya ukuaji na ushirikiano wa kikanda,” alisema.
Waziri wa Kawi Opiyo Wandayi pia ameahidi kuongoza kampeni za kumrejesha Rais Ruto mamlakani mwaka 2027, akisema hatua hiyo inaendana na maono ya Raila Odinga.
Hata hivyo, bado haijabainika ikiwa Gavana wa Siaya James Orengo atakuwepo kumpokea Rais wakati wa uzinduzi wa miradi katika maeneo ya Bondo na Gem.