Tamko la Kindiki lamtosa kwenye tope aliloogelea mdosi wake
NAIBU Rais Kithure Kindiki amedhihirisha uaminifu wake wa dhati kwa Rais William Ruto akimuunga kwa kuwarushia cheche kali wapinzani wake wa kisiasa kwa kumkosoa.
Akizungumza Jumatano, Machi 18, 2026, akiwa katika Kaunti ya Bomet, Kindiki aliwashutumu viongozi wa upinzani na wakosoaji wa rais kwa kutumia muda wao kuwatukana viongozi badala ya kuwasilisha sera wazi kwa Wakenya.
Kulingana na Kindiki, na usisahau ni profesa, wakosoaji hawawezi kumtaka Rais Ruto ambaye anakumbusha wapinzani kwamba amesomea uzamifu, kuonyesha mwenendo unaostahili ofisi yake ya urais ilhali wao wenyewe hawamheshimu yeye na ofisi anayoshikilia.
“Badala ya kusema sera yenu, mmetumia muda wenu wote kutukana, kudharau na kudhalilisha Rais wa Taifa la Kenya. Mimi nawauliza hivi, kabla ya kuanza kudai Rais Ruto anafaa kuwa na mienendo ya urais, je, mmemchukulia kama rais? Munamtaja na kumheshimu kama Rais wa Kenya kabla ya kuanza kusema lazima akae kama rais?” alihoji Kindiki.
Aliongeza kuwa haiwezekani kumtaka rais kuonyesha hadhi ya urais ilhali wakosoaji wamekuwa wakimkashifu yeye pamoja na ofisi ya urais.
“Hauwezi kudai Rais Ruto anafaa kuwa na mienendo ya urais wakati mmetumia muda wenu wote kumtukana na kudhalilisha ofisi ya rais pamoja na anayeshikilia ofisi hiyo. Na mimi nimesema inatosha. Nimemwambia mdosi wangu sasa atulize boli. Awachane na hawa watu kwa sababu ni watu wadogo kisiasa. Awachie sisi tutawashughulikia hawa wahusika,” alisema.
Aliwapuuza baadhi ya wakosoaji akisema wengi wao hawana uzito mkubwa kisiasa.
“Sisi tumepigana vita kubwa. Hii dharau dhidi ya Rais Ruto imetoka wapi? Mimi nimemwambia mdosi wangu atuachie hawa watu. Hawa ni watu wadogo kisiasa. Wengine hawajakuwa chochote. Wengine wamekuwa wabunge wa muhula mmoja tu na hawajafanya kazi nyingine yoyote duniani,” alisema.
Alitoa kauli hizo wakati wa malumbano makali kati ya Rais Ruto na baadhi ya viongozi wa upinzani, akiwemo aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua ambayo yamejumuisha mashambulizi ya kibinafsi kuhusu mwonekano na maisha ya viongozi, jambo lililozua mjadala kuhusu iwapo rais alishusha hadhi ya ofisi yake au alijibu uchokozi. Kindiki alisisitiza kuwa ukosoaji huo si wa haki na akawahimiza wakosoaji kuangazia ajenda zao badala ya kumshambulia rais kwa maneno.