Kimataifa

Amerika, EU wapinga fidia kwa Afrika kwa dhuluma za kuuzwa utumwani miaka ya kale

Na REUTERS March 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

NEW YORK, AMERIKA

PENDEKEZO la Ghana katika Mkutano wa Baraza la Umoja wa Mataifa (UNGA) kutambua utumwa na dhuluma dhidi ya Waafrika kama uhalifu mbaya zaidi wa kibinadamu jana lilipitishwa licha ya Amerika na Ulaya kupinga.

Ghana kwenye pendekezo hilo inataka uhalifu huo utambuliwe kisha mataifa ya Afrika yalipwe fidia kutokana na dhuluma hizo.

Rais wa Ghana John Mahama alisema pendekezo hilo lilihitaji kupitishwa ili Waafrika watendewe haki.

Hii ni kwa sababu zaidi ya Waafrika milioni 12.5 walipelekwa katika utumwa na kufanyishwa kazi za sulubu katika karne ya 15 na 19.

Mahama alisema hadi leo utumwa huo umesababisha bara hili libaguliwe na pia kushamiri kwa ubaguzi wa rangi.

Waziri wa Masuala ya Nje wa Ghana Samuel Abalakwa alisema kuwa pendekezo hilo lilikuwa likisisitizia tu uwajibikaji na Afrika kutendewa haki kutokana na dhuluma ambazo ilipitishiwa.

Katika mkutano wa UNGA, nchi 123 ziliunga mkono pendekezo hilo ambalo sasa linaonekana kuwa na uzito wa kisiasa kwa waliolipinga.

Amerika na Israel zilikataa kushiriki kura hiyo pamoja na Muungano wa Bara Ulaya (EU) na Uingereza.

Katibu Mkuu wa Baraza la Umoja wa Kitaifa Antonio Guterres aliambia UNGA kuwa juhudi zaidi zilihitajika kukabili dhuluma za kihistoria.

Hadi leo, Uholanzi ni nchi pekee ambayo iliomba msamaha kutokana na jinsi ilivyowanyanyasa Waafrika kupitia biashara ya utumwa.

EU na Amerika zilipinga pendekezo hilo zikisema kuwa litaweka mpaka kuwa aina moja ya uhalifu ni katili kuliko mwingine na pia zikapinga Afrika kutumia ukatili uliofanyika miaka mingi iliyopita kusaka fidia.