Uncategorized

Siasa za urithi: Makataa ya ODM Takwa tata la ODM kwa UDA kuhusu ugombeaji

Na BENSON MATHEKA March 29th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

CHAMA cha Orange Democratic Movement (ODM) kimeashiria msimamo mkali kuhusu suala la kutengewa maeneo ya uchaguzi huku Mkutano wake Maalum wa Wajumbe (SDC) ukiidhinisha rasmi kuendelea kwa mazungumzo ya kisiasa na chama cha United Democratic Alliance (UDA).
Hatua hii inaweka msingi wa mabadiliko makubwa ya kisiasa kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027 huku wadadisi wa siasa wakisema huenda ikawa ngumu kwa UDA kukubali takwa hilo.
Kiini cha mvutano huu wa kisiasa ni mzozo kati ya vyama hivyo viwili kuhusu kutengewa maeneo, mbinu ya kuachia kila chama maeneo maalumu ili kuepuka kugawanya kura.
Ingawa ODM inaonekana kutaka kulinda ngome zake za jadi kupitia mkakati huo, viongozi wa UDA wanapinga vikali, wakisisitiza ushindani wa wazi katika maeneo yote ya uchaguzi.
SDC hiyo iliyofanyika Ijumaa, katika uwanja wa Jamhuri, iliwaleta pamoja wajumbe wa ODM na viongozi wa juu kupanga mustakabali wa chama hicho. Hapo ndipo Kiongozi wa Wachache katika Bunge la Kitaifa, Junet Mohamed, alitoa ujumbe mkali: ODM haitakubali nguvu zake bungeni zidhoofishwe katika mazungumzo yoyote.
“Tunalenga kuongeza idadi yetu katika Uchaguzi Mkuu ujao kutoka ilivyo sasa. Tunataka kuambia chama chochote tutakachoshirikiana nacho kuwa idadi yetu bungeni haiwezi kujadiliwa. Tunaweza kujadili chochote, lakini si nguvu yetu bungeni,” alisema Junet.
Kauli yake inaakisi mkakati mpana wa ODM wa kuingia katika muungano wowote ikiwa na nguvu ya kutosha kisiasa. Chama hicho kinachukulia uwepo wake bungeni kama silaha ya majadiliano na pia kinga dhidi ya kutengwa kisiasa.
Viongozi wenye ushawishi wanataka ngome za chama zilindwe. Mbunge wa Homa Bay Town, Peter Kaluma, alisema kutengewa maeneo ni muhimu ili kudumisha ushawishi wa ODM.
“Ni lazima tuhakikishe ngome zetu za msingi zinalindwa na kuachiwa ODM, na kutengewa maeneo kutafanyika. Bila hilo, hatutakuwa na makubaliano,” alisisitiza.
Lakini katika upande wa UDA, viongozi wanapinga vikali wazo hilo. Katibu Mkuu wa chama hicho, Hassan Omar, alisema demokrasia lazima itangulizwe badala ya makubaliano ya kulindana kisiasa.
“Hakutakuwa na kutengewa maeneo, na kila mmoja atalazimika kujitafutia ushindi. Wenye kura tatu walete, wenye kura 300 walete. Hakuna sababu ya kuwa na hofu kama hiyo ndiyo nguvu yako,” alisema.
Kwa upande wake, Mbunge wa Molo, Kimani Kuria, alikosoa hatua hiyo akisema inakwamisha ukuaji wa demokrasia.
Wakati huo huo, Rais William Ruto anaendelea kuimarisha nguvu zake za kisiasa kupitia UDA ili kuongeza nafasi yake ya kuchaguliwa tena mwaka 2027.
Wachanganuzi wa siasa wanasema katika muktadha huu, msimamo wa ODM kuhusu kutengewa maeneo unaonyesha wasiwasi wa ndani kuhusu uhai wa kisiasa na ushawishi wake.
Wanaounga mkono takwa hili ni mbinu ya kulinda maslahi yao kwanza na ya chama ili wasishindwe na wale wa UDA hasa baada ya ushawishi wa chama hicho cha chungwa kuyumba kufuatia kifo cha mwanzilishi wake Raila Odinga mwaka jana.
“Mazungumzo kati ya ODM na UDA yanapoendelea kushika kasi, suala la kutengewa maeneo linazidi kuwa jaribio kuu ambalo itabidi Dkt Oburu afanya kazi ya ziada kushinda ikizingatiwa nguvu za mshirika wake katika serikali Jumuishi, Rais William Ruto,” asema mdadisi wa siasa Dkt Isaac Gichuki.
Tayari, Rais Ruto ameashiria kuwa chama chake cha UDA na ODM vitashiriki katika ushindani wa “kirafiki” katika Uchaguzi Mkuu wa 2027, akidokeza mwisho wa siasa za kutenga maeneo ya ushindani.
Iwapo vyama hivi viwili vitaweza kupatanisha misimamo yao tofauti, huenda ndilo litakaloamua mwelekeo wa siasa za nchi kuelekea mwaka 2027.
UDA kimetangaza kuwa kitawania viti vyote vilivyo wazi, hatua inayokinzana na msimamo wa ODM wa kutaka maeneo yake ya kisiasa yahifadhiwe kupitia mfumo wa kugawa maeneo ya ushindani.