Iran yashambulia meli licha ya vitisho vya Trump
TEHRAN, IRAN
IRAN Jumanne, Machi 31, 2026 ilishambulia na kuteketeza meli yenye mafuta ghafi licha ya vitisho vya Rais wa Amerika Donald Trump kuwa itashambulia viwanda na vituo vyake vya kawi.
Trump alitoa vitisho hivyo ili kushinikiza Iran iruhusu meli zipite Strait of Hormuz ambapo zaidi ya asilimia 20 ya mafuta ulimwenguni hupitia.
Alisema Amerika itavishambulia viwanda na vituo vya kawi ambavyo Iran huuzia mafuta yake kwa nchi nyingine ulimwenguni.
Meli hiyo kwa jina Al-Salmi ilikuwa ya Kuwait na nahodha na waliokuwa ndani walinusurika.
Shirika la Mafuta la Kuwait lilithibitisha kuwa meli hiyo iliharibiwa vibaya kutokana na shambulizi la Iran.
Tangu vita kati ya Amerika-Israeli dhidi ya Iran vianze mnamo Februari 28, Iran imekuwa ikidhibiti meli zinazopitia Strait of Hormuz.
Hatua hiyo imesababisha bei ya mafuta kupanda sana ulimwenguni huku mataifa mengi yakianza kukumbwa na ukosefu wa bidhaa hiyo muhimu.
Takwimu zinaonyesha kuwa meli hiyo ilikuwa ikielekea Qingdao, China na ilikuwa imebeba mapipa milioni 1.2 ya mafuta ghafi.
Pia kulikuwa na mapipa 800,000 ya mafuta ghafi ya Kuwait.
Ingawa hivyo, huenda Iran haikuwa inalenga Al Salmi kwa sababu wanajeshi wa Iran walisema walikuwa wakilenga meli moja ya shehena ukanda wa Gulf ambayo ilikuwa na uhusiano na Israeli.
Wanajeshi hao walionekana wakirejelea Meli ya Haiphong Express ya Singapore ambayo ilikuwa imetua karibu na Al Salmi.
Ghasia kati ya Amerika-Israel na Iran zimeenea katika ukanda wa Mashariki ya Kati ambapo wengi wameuawa na kujeruhiwa.
Pia usambazaji wa mafuta umeathirika na uchumi wa ulimwengu kutikiswa.
Vita hivyo, havionekani kama vitakavyoisha hivi karibuni ingawa Pakistan imejitolea kuwa mpatanishi.
Waziri wa Mashauri ya Kigeni Pakistan Ishaq Dar, alikuwa azuru China mnamo Jumanne baada ya kuandaa mazungumzo na Uturuki, Misri na Saudi Arabia.
China ni mshirika wa Iran na mnunuzi mkubwa zaidi wa mafuta yake, ilitoa wito kwa pande zote zinazohusika na vita hivyo, zikumbatie mazungumzo.
Hivi majuzi Iran iliruhusu meli tatu za mafuta za China kupitia Strait of Hormuz huku Iran ikiapa kuwa haiwezi kurejelea mazungumzo na Amerika.
Trump hivi majuzi alidai kuwa Amerika inazungumza na viongozi wapya wa Iran ambao wamerithi nafasi ya wale ambao waliuawa vitani.
Hata hivyo, alitoa onyo kuwa Iran ikikataa kufungua Mkondo wa Hormuz sasa italenga vituo vikubwa vya kawi ambavyo Iran hutumia kuyauza mafuta yake kwa mataifa mengine duniani.
Amerika tayari imeanza kukumbwa na uhaba wa mafuta huku suala hilo likisababisha umaarufu wa Trump kupungua.
Haya yanajiri siku chache baada ya Trump kusema kuwa viongozi wapya wa Iran “wanatumia akili zao vizuri”.
Alisema hayo wakati ambapo wanajeshi wa Amerika waliwasili Mashariki ya Kati na Iran ikaonya kuwa haitakubali kukandamizwa.