Gavana Nassir, Shahbal kung’ang’ania tikiti ya ODM kuelekea 2027
VIGOGO wawili wote wakiwa na ushawishi mkubwa katika chama cha ODM mjini Mombasa wote wakiwania kiti cha ugavana katika uchaguzi mkuu wanahofiwa kugawanya chama iwapo mchujo wa uteuzi huo hautafanywa kwa njia ya uhuru na haki.
Gavana wa sasa ambaye pia ni naibu kinara wa chama cha ODM Abdulswamad Nassir na mfanyibiashara mashuhuri ambaye pia ni mbunge wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Bw Suleiman Shahbal wote wanawania kiti cha ODM huku wote wakionekana na nafasi sawa za kupata nafasi hiyo.
Hata hivyo, wachanganuzi wa siasa wanahofia kuwa iwapo mchujo wa uteuzi wa mgombeaji ambaye atapeperusha bendera ya ODM Mombasa, chama hicho kinaweza pata pigo na kugawanya chama hicho zaidi na kupunguza umaarufu wa chama hicho.
Bi Maimuna Mwidau, mchanganuzi wa siasa eneo la Pwani alisema lazima chama hicho kuwa makini ikizingatiwa Gavana Nassir tayari yuko kwa meza ya kupanga wawaniaji huku Bw Shahbal ako na ushawishi kwa wananchi na siasa za kitaifa.
Bi Mwidau alisema kutangaza kwa Bw Shahbal kuwa wakati huu hatajiuzulu na atagombea kiti cha Mombasa kwa tikiti ya ODM, kumeongeza hofu kwa chama kwani lazima wawe na umoja iwapo wanataka kushinda kiti hicho cha ugavana.
“Bw Shahbal ako na wafuasi wengi na amekuwa na ushawishi kibiashara na kisasa ngazi za juu, na hilo litamsaidia kuwania kiti hicho lakini Gavana Nassir ako kwa chama na viongozi wengine hawawezi kumnyima tikiti ya kuwania awamu yake ya pili. Swali kuu litakuwa nani atachukua tiketi hiyo?,” aliuliza Bi Mwidau.
Hivi karibuni, Bw Shahbal ameonekana akiwa na ukaribu na aliyekuwa Gavana wa Mombasa ambaye kwa sasa ni Waziri wa Madini na Uchumi Baharini Ali Joho ambaye ana ushawishi mkubwa wa siasa sio tu Kaunti ya Mombasa bali eneo nzima la Pwani.
Bi Mwidau hata hivyo alisema kwa sasa Bw Joho na Shahbal kwa sasa ni wanachama na hawakai kwa meza ya kufanya uwamuzi hivyo basi itakuwa vigumu kutoa Bw Nassir.
Bw Ali Karissa, mkazi wa Mombasa alisema siasa za mwaka ujao zitakuwa ngumu kwa ODM ikizingatiwa mchujo peke yake unaeza kulazimu wengine kujitoa kwa chama.
“Iwapo Shahbal na Gavana Nassir wanaenda mchujo, mmoja wao lazima akubali kuungamshindi mkono iwapo atashindwa ili kutosambaratisha chama hicho kama wanataka kupata ushindi,” alisema Bw Larissa.
Bw Shahbal amekuwa mshiriki mkuu katika siasa za Mombasa na ugavana na amekuwa na uungwaji mkono mkubwa lakini kujiondoa kulikera wafuasi wake pakubwa.
Bw Shahbal ambaye anawania kiti hicho kwa mara ya tatu mapema mwaka huu alikiri kuwa aliwasaliti wafuasi wake baada ya kukubali wito wa aliyekuwa kiongozi wa chama cha ODM hayati Raila Odinga na aliyekuwa rais, Bw Uhuru Kenyatta kuacha azma yake kuwa gavana hivyo basi anakibarua kigumu kuwashawishi wapigaji kura kusahau yaliyopita na kumuunga mkono.
Bw Shahbal alijitosa katika kinyang’anyiro cha ugavana wa Mombasa mwaka 2013 na 2017 na katika uchaguzi mkuu wa 2022 na alikuwa na nia ya kuwania kiti cha ugavana wa Mombasa chini ya chama cha ODM.
“Najua kuna wafuasi wangu wengi sana ambao walikasirika sana nilipojiondoa kwenye kinyang’anyiro hicho. Naomba msamaha kwani kujiondoa kwangu nilipata shinikizo kutoka kwa viongozi hao wawili,” alisema Bw Shahbal.
Hata hivyo, Bw Shahbal anajitosa katika uwanja ambao wawaniaji zaidi ya watano wametangaza nia yao ya kugombea kiti cha ugavana.
Viongozi hao wameanza kunowa makali yao huku wakimkashifu Bw Nassir kwa madai ya kutotekeleza miradi ya kuboresha maisha ya wakazi hao.
Mbunge wa Nyali Mohammed Ali tayari ameanza kukupigia debe licha ya kuwa na upinzani mkali akilaumu viongozi katika Kaunti ya Mombasa kumnyima nafasi ya kujitangaza na kuhamasisha wakazi kuandikisha Kura.
Wiki hii, Bw Ali akikashifu uongozi wa Kaunti ya Mombasa kwa kutoa mabango take aliyoweka kwa barabara ya kushawishi wakazi kujiandikisha kura.
Katibu mkuu wa UDA Bw Hassan Omar ambaye ni mwandani wa Raisi William Ruto mjini Mombasa na kuungana kwa chama cha UDA na ODM kwa serikali kumezidi kumpa nafasi zaidi ya kujizolea kura katika Kaunti hiyo ambayo inaonekama kupungua kwa wafuasi wa upinzani wa ODM.
Bw Omar alipoteza kiti cha Ugavana kwa kupata kura 98,105 dhidi ya gavana wa sasa Nassir wa ODM aliyepata kuwa 119,083 licha ya kuungwa mkono na aliyekuwa gavana wa Nairobi Mike Sonko na viongozi wengine.
Spika wa bunge la kaunti ya Mombasa Aharub Khatri naye ako mbioni kusaka kiti hicho.
Hata hivyo, Gavana wa sasa Bw Nassir anatumia ushawishi wake wa chama cha ODM kuzidi kujiongezea umaarufu na anajivunia kukamilisha miradi mbalimbali ambayo aliyekuwa Gavana Joho alianzisha na kuzindua kadhaa.
Wengine ambao wanamezea mate kiti hicho ni pamoja na aliyekuwa mbunge wa Kisauni Ali Mbogo.