Gachagua adai serikali imeunda kikosi maalum kuvuruga upinzani uchaguzi ukikaribia
KIONGOZI wa chama cha Democracy for the Citizens Party (DCP), Rigathi Gachagua, jana aliishambulia serikali, akiishutumu kwa kutumia idara za usalama kuvuruga mikutano ya kisiasa ya muungano wa upinzani.
Bw Gachagua alilaani maafisa wa usalama kufuatia vurugu katika mkutano wake eneo bunge la Kikuyu, Kaunti ya Kiambu, Jumamosi, ambapo polisi walirushia vitoa machozi viongozi na wafuasi.
Kabla ya tukio hilo, barabara zinazoelekea mji huo zilidaiwa kufungwa na makundi ya wahuni.
“Serikali imeunda upya kikosi cha polisi cha maafisa 12 kilichotushambulia Witima miezi kadhaa iliyopita na bado kinaendelea kufanya kazi bila kuchukuliwa hatua. Ni kikosi hicho hicho kilichotushambulia Kikuyu Jumamosi,” alisema Bw Gachagua.
Bw Gachagua alidai kuwa vitendo hivyo vinaashiria njama pana ya kuwanyamanzisha viongozi wa upinzani na kuzuia mikutano yao kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Alisisitiza kuwa licha ya changamoto hizo, wataendelea kutumia njia za kikatiba katika kupigania mabadiliko ya kisiasa nchini.
Bw Gachagua pia alimkosoa Rais William Ruto, akisema Waziri wa Usalama wa Ndani Kipchumba Murkomen hafai kushikilia wadhifa huo, akidai wizara hiyo imegeuzwa kuwa chombo cha kisiasa badala ya kulinda usalama wa wananchi.
Bw Gachagua alizungumza katika eneo la Kajiado Kati wakati wa ibada katika kanisa la PEFA Works akiandamana na kiongozi wa DAPK Eugene Wamalwa, aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiang’i, maseneta Samuel Seki (Kajiado), Dan Maanzo (Makueni), John Kinyua (Laikipia), Karungo wa Thang’wa (Kiambu) pamoja na wabunge na madiwani kadhaa.
“Tunaheshimu Katiba. Hata kama mmeiharibu nchi, bado tunaamini katika utawala wa sheria. Tuko tayari kusubiri miezi 14 iliyosalia kuwaondoa kupitia kura,” alisema.
Bw Wamalwa alishutumu polisi kwa kushirikiana na wahuni kuvuruga mikutano ya upinzani kote nchini, akisema hali hiyo inahatarisha demokrasia na uhuru wa kujieleza.
Dkt Matiang’i, ambaye aliwahi kuhudumu katika wizara hiyo wakati wa utawala wa Rais mstaafu Uhuru Kenyatta, alimkosoa mrithi wake akisema wizara hiyo imeingizwa siasa na kupoteza mwelekeo wake wa kitaaluma.
“Katika sekta ya usalama kuna kinachoitwa tathmini ya vitisho. Kila asubuhi viongozi wa usalama humfahamisha Waziri kuhusu vitisho kwa taifa. Tishio haliwezi kuwa Rigathi Gachagua anayezungumza na wafuasi wake. Kutumia polisi na rasilimali za umma kuvuruga mikutano ya kisiasa ni kupoteza fedha za walipa ushuru,” alisema.
Seneta wa Kajiado Samuel Seki alisema maafisa wa usalama walitumika kuvuruga mikutano ya barabarani katika maeneo ya Isinya, Kiserian na Ngong, akiongeza kuwa hali ya taharuki bado ipo huku wafuasi wa upinzani wakihofia usalama wao.
“Hii ni moja ya kaunti zilizo na ahadi nyingi ambazo hazijatekelezwa. Tunajua kuna juhudi za kuvuruga mikutano yetu lakini tuko tayari kukabiliana na hali hiyo,” alisema.
Hata hivyo, Kamanda wa Polisi Kaunti ya Kajiado, Alexander Shikondi, alikanusha vikali madai hayo akisema si kweli kwamba polisi wanahusika na vurugu au kupanga mashambulizi dhidi ya raia.
“Ni jambo la kusikitisha kwa yeyote kudai kuwa Huduma ya Polisi ya Kitaifa inaweza kupanga au kutekeleza vurugu dhidi ya Wakenya. Hilo si jukumu letu, na pia si sahihi kimaadili kuwataja maafisa hadharani bila ushahidi,” alisema.
Aliongeza kuwa baadhi ya wanasiasa wamekuwa wakitoa madai mazito hadharani lakini hawatoi malalamishi rasmi kwa polisi ili yafanyiwe uchunguzi.
“Ni vigumu kuchunguza madai ambayo hayajaripotiwa rasmi. Wito wetu ni kwa yeyote aliye na ushahidi kutoa taarifa ili hatua zichukuliwe kwa mujibu wa sheria,” alisema.