Babu Owino apatia upinzani siri ya kubwaga Ruto 2027
Mbunge wa Embakasi Mashariki, Babu Owino, amesema kuwa iwapo upinzani hautaungana, Rais William Ruto anaweza kushinda uchaguzi wa 2027 kwa asilimia 100.
Akizungumza katika mahojiano kwenye podcast ya mchanganuzi wa siasa, Herman Manyora iliyopeperushwa Jumapili, Aprili 12, 2026, mbunge huyo ambaye pia ni miongoni mwa wanaomezea mate ugavana kaunti ya Nairobi katika uchaguzi mkuu wa mwaka ujao, alisema umoja wa vinara wa upinzani ndiyo njia pekee ya kumshinda Rais Ruto.
Babu alisema kuwa iwapo kila kiongozi wa upinzani ataamua kugombea kivyake, kura zitagawanyika na kumpa Rais Ruto ushindi rahisi.
“Iwapo upinzani utaungana, watashinda kwa asilimia 100. Wasiwe na ubinafsi; kila mmoja awe tayari kuacha azma yake kuunga mwingine,” alisema.
Vinara wa muungano wa upinzani wameapa kuweka kando azma zao za binafsi na kumuunga mkono mgombea mmoja dhidi ya Rais Ruto katika uchaguzi ujao.
Vuguvugu la Linda Mwananchi, ambalo Babu Owino ni mmoja wa waanzilishi, pia imeonyesha nia ya kushirikiana na upinzani ili kufanikisha lengo lao la kumfanya Rais Ruto kuwa kiongozi wa muhula mmoja.
Kiongozi wa vuguvugu hilo, Edwin Sifuna, alikuwa wa kwanza kuashiria kuwa yuko tayari kufanya kazi na vinara wa upinzani, akisema kwamba ushindi dhidi ya Ruto utahitaji mshikamano wa kisiasa.
Kulingana na Sifuna, hataki kuwa sehemu ya kugawanya kura kama ilivyotokea katika chaguzi zilizopita, akihimiza umoja dhidi ya Ruto.
Kauli kama hiyo imeungwa mkono pia na Seneta wa Vihiga, Godfrey Osotsi, ambaye amesema ingawa bado ni mapema kuzungumzia makubaliano rasmi, hatimaye pande hizo mbili zitashirikiana.
Gavana wa Siaya, James Orengo, naye ameendelea kusisitiza umuhimu wa umoja wa upinzani.
Kwa upande mwingine, muungano wa upinzani umeonyesha nia ya kushirikiana na Linda Mwananchi, ukisema utaunga mkono mgombea wa pamoja mwenye nguvu ya kushinda Rais Ruto.
Muungano wa upinzani unawaleta pamoja kinara wa chama cha DCP Rigathi Gachagua, Kalonzo Musyoka wa chama cha Wiper, Martha Karua wa Peoples Liberation Party,Fred Matiang’i wa chama cha Jubilee, Eugene Wamalwa wa chama cha DAP- Kenya na Justin Muturi wa Democratic Party.
Vinara hao wamekuwa wakifanya mikutano ya kisiasa wakilenga kushirikiana kushindana na muungano tawala wa Kenya Kwanza na Serikali Jumuishi inayopigwa jeki na chama cha ODM kinachoongozwa na Dkt Oburu Oginga.
Mbunge wa Kitutu Chache Kusini, Antony Kibagendi, amesema kuwa Rais William Ruto tayari amekubali hali ya kisiasa inayoashiria uwezekano wa kushindwa katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Katika taarifa aliyochapisha kwenye mitandao yake ya kijamii Aprili 13 2026, Kibagendi alidai kuwa mwenendo wa kisiasa wa hivi karibuni na viashiria vya maoni ya wananchi vinaonyesha kuwa Rais anakabiliwa na safari ngumu ya kisiasa kuliko ilivyokuwa wakati alipoingia madarakani.
Kwa mujibu wake, licha ya Rais kuonekana kuwa na uungwaji mkono kitaifa, takwimu za sasa hazionyeshi kiwango kinachoweza kumhakikishia ushindi wa duru ya kwanza chini ya masharti ya uchaguzi wa Kenya.
“Inazidi kudhihirika kwamba Rais William Ruto anatambua kikamilifu mlima mrefu wa kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027,” alisema Kibagendi.
Alidai zaidi kuwa tafiti mbalimbali za maoni ya wananchi zilizofanywa na taasisi kama Huduma ya Kitaifa ya Ujasusi (NIS), Baraza la Makanisa la Kitaifa la Kenya (NCCK), Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya (KCCB), pamoja na kampuni za utafiti kama Infotrak , zinaonyesha mabadiliko ya hisia za kisiasa nchini.