Kalonzo ashinikizwa amteue Sifuna mgombea mwenza 2027
WAJUMBE wa chama cha Wiper Patrotic Front katika eneo la Pwani, wamemhimiza kinara wao Kalonzo Musyoka amteue Seneta wa Nairobi, Bw Edwin Sifuna, kuwa mgombea mwenza katika uchaguzi mkuu ujao.
Akiongea kwa niaba ya viongozi hao wakiongozwa na Mbunge wa Wundanyi, Bw Danson Mwashako, ambaye anawania ugavana kupitia Wiper, viongozi hao walisema Bw Sifuna atasaidia mrengo wa upinzani kuvutia kura za vijana maarufu wa Gen Z.
“Tunajua Bw Musyoka ndiye atakayepeperusha bendera ya urais kupitia Upinzani na tunamwomba amchague Bw Sifuna kuwa naibu wake kwenye kinyang’anyiro hicho ilia apate kura za vijana,” alisema Bw Mwashako kwenye mkutano wa Wiper katika uwanja wa shule ya Taita Academy.
Bw Mwashako aliwaonya wakazi dhidi ya kushurutishwa kujiunga na UDA.
Kwa upande wake, Bw Musyoka, aliwakumbusha wakazi wa Kaunti hiyo kuwa katika uchaguzi uliopita, chama cha Wiper kilivuna viti vingi Taita Taveta, ambapo kilipata wabunge watatu kati ya wanne na madiwani kadhaa.
Alisema Kaunti hiyo imekuwa ngome ya Wiper tangu 2017 ilipochagua Gavana Granton Samboja kupitia tikiti ya chama hicho.
Bw Samboja aliangushwa mwaka 2022 na Gavana Andrew Mwadime, lakini sasa amejiunga na UDA na anapania kuwania useneta.
“Bw Samboja alikuwa kijana wangu lakini sasa sijui yuko upande gani. Hata hivyo, bado tunamkaribisha. Nitarudi tena hapa kufanya kampeni nikiwa na Rigathi Gachagua (DCP), Eugene Wamalwa (DAP-K), Bw Justine Muturi, Bw Fred Matiangi na wengineo,” alisema Bw Musyoka.
Kuhusu Bw Sifuna, Bw Musyoka aliwahakikishia wakazi kwamba wako mrengo mmoja lakini kwa sasa bado anasubiri kumaliza changamoto katika chama cha ODM kabla ya kujiunga nao.
“Sifuna atakuja bila shaka, sisi ni timu moja, sisi ni wana Wan Tam. Lakini kwa sasa kuna kazi muhimu anataka kusuluhisha ndani ya ODM. Ile ODM yangu na marehemu Raila Odinga tulianzisha ODM Kenya tukagawanywa sasa imegawanywa tena. Kuna ODM imenunuliwa na Bw Ruto lakini Bw Sifuna na wenzake wamekataa, wakisuluhisha bila shaka tutaungana pamoja,” alisema Bw Musyoka.
Bw Musyoka alisema mwaka jana aliidhinishwa kuwa mgombea wa chama cha Wiper kwa uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.
“Chunga kura yako ili tumpige risasi moja kupitia debe, tulipize kisasi kwenye uchaguzi mkuu,” alisema Bw Musyoka.
Alisema sekta ya elimu imedorora kufuatia uongozi mbaya wa Rais Ruto huku wanafunzi wengi wakiacha shule kufuatia changamoto ya karo ya shule.
Bw Mwashako alimshukuru Musyoka kwa kukuza viongozi wa Wiper kisiasa katika kaunti hiyo, akitaja changamoto kubwa ya ardhi ambayo imekuwa dondasugu.
Alisema mashamba yanaendelea kunyakuliwa na mabwenyenye huku wakazi wakiachwa bila makao, akitoa mfano wa Taveta na Voi ambapo wakazi walifurushwa na nyumba kubomolewa.
“Tumebakia na mwaka mmoja na miezi minne. Tunakuomba Bw Musyoka, ukipata uongozi, utunge tume maalum ya kuchunguza unyakuzi wa ardhi,” alisema.
Aidha, aliwaonya wakazi dhidi ya kumshabikia Rais William Ruto akisema ameshindwa kutatua changamoto zinazowakabili, ikiwemo kugawanya mapato kutoka mbuga ya Tsavo, ajira katika Shirika la Huduma ya Wanyamapori na upatikanaji wa maji kutoka chemi chemi ya Mzima.
Mbunge wa Voi, Bw Abdi Chome, aliongeza kuwa Wiper inazidi kupata umaarufu kutokana na maadili bora ya uongozi.