Lugha, Fasihi na Elimu

Swali mwigo katika tamthilia ya ‘Bembea ya Maisha’

April 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

LEO naomba tuangazie swali hili katika tamthilia ya ‘Bembea ya Maisha.’

Sara, nyumba hii haifuki walau moshi hata kama chakula ni taabu kwako? Yona mume wangu, moshi utafukaje?

Mwenzio hapa nilipo kichwa kimeudara mto siku nzima. Wewe unajua ni kwa ajili ya maradhi haya; si kwa uzembe wala raha.

Miaka yote hiyo nikiwa ningali mzima na afya yangu mbona sikufanya ajizi? Muda huo wote nikipika mimi, nikiandaa na kukukaribisha ule.

Iweje leo kazi hiyo inishinde? Basi mbona usimwite bintiyo akaja kukupeleka hospitalini?

Huyo mtoto naye pamoja na mzigo wa familia yake amejaribu kiasi chake. Amewafaa wanuna wake kwa hali na mali.

Kulipia elimu ya chuo kikuu si lelemama. Kutoa ni moyo, usambe utajiri.

Sharti ujue kwamba fimbo ya mzee hurithi mtoto wa kwanza…hukumbuki kwamba alituajiria wafanyakazi kutusaidia…hata sasa umetumia mapeni uliyotumiwa kwenda kwa wazee wenzio ili wasikuone shabiki…nimempelekea Dina salamu aje akatufanyie chochote.

i) Chambua mtindo katika kifungu kifuatacho.
Taswira – Nyumba hii haifuki walau moshi
Tashihisi – kichwa kimeudara mto siku nzima
Mbinurejeshi – Miaka yote hiyo nikiwa ningali mzima na afya yangu mbona sikufanya ajizi?
Methali – Kutoa ni moyo, usambe ni utajiri
Istiara – fimbo ya mzee hurithi mtoto wa kwanza
Takriri – walau moshi, moshi utafukaje?
Tasfida – wazee wenzio ili wasikuone shabiki…

ii) Jadili baadhi za sifa za wahusika katika kifungu hiki.

YONA
Mwenye mapuuza – Nyumba hii haifuki walau moshi hata kama chakula ni taabu kwako? Anapuuza hali ya ugonjwa ya Sara na kutaka ampikie.
Mbinafsi – hata kama chakula ni taabu kwako? Hajali hali ya Sara ya kutoweza kula chakula. Kwake Yona kula chakula si taabu lakini Sara anapata taabu alapo.
Mnafiki – Wewe unajua ni kwa ajili ya maradhi haya; si kwa uzembe wala raha. Kwa hivyo Yona anajua ni kwa ajili ya maradhi yanayosababisha kutopikiwa.
Mtamaduni – Sharti ujue kwamba fimbo ya mzee hurithi mtoto wa kwanza…

SARA
Mwenye heshima kwa mumewe- Mume wangu, moshi utafukaje? Mwenzio hapa nilipo kichwa kimeudara mto siku nzima.
Mwenye bidii – Wewe unajua ni kwa ajili ya maradhi haya; si kwa uzembe wala raha.
Mwenye kuwajibika – Muda huo wote nikipika mimi, nikiandaa na kukukaribisha ule.
Mwenye shukrani – Huyo mtoto naye pamoja na mzigo wa familia yake amejaribu kiasi chake.
Mwenye busara – Nimempelekea Dina salamu aje akatufanyie chochote.

DINA
Mwenye kuwajibika – nimempelekea Dina salamu aje akatufanyie chochote. Yeye huitikia wito haraka.

iii) Tambua aina za urudiaji katika kifungu hiki.
Urudiaji wa silabi – moshi, moshi,
Urudiaji wa neno -moshi, moshi

iv) Tambua toni katika kifungu hiki
i) Toni ya malalamishi – Nyumba hii haifuki walau moshi hata kama chakula ni taabu kwako?
ii) Toni ya heshima – Mume wangu, moshi utafukaje? Mwenzio hapa nilipo kichwa kimeudara mto siku nzima.
iii)Toni ya kutamauka – Mwenzio hapa nilipo kichwa kimeudara mto siku nzima.