Makala

Kamari ilivyoharibu ladha ya ushabiki wa michezo: ‘Unajikuta ukiombea timu yako ishindwe’

Na CELLESTINE OLILLO April 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

JUZI, nilikuwa nimetulia katika baa moja kwenye barabara ya Ngong nikifurahia kinywaji baridi huku nikitazama mechi kati ya Arsenal na Manchester City.

Kwangu, kunywa kinywaji huku nikitazama mechi peke yangu ni moja ya raha kubwa maishani—kwa saa mbili, dunia nzima hupotea akilini.

Hata hivyo, hali ilibadilika jioni hiyo kundi la wanaume lilipowasili kutazama pambano lililokuwa likisubiriwa kwa hamu kati ya Liverpool na Nottingham Forest.

Tulianza mazungumzo ya kawaida kabla ya mechi kuanza—kuhusu wachezaji wapya na nafasi ya Arsenal kushinda ligi.

Lakini mmoja wao, shabiki wa Liverpool, alikuwa ameweka beti (dau) kubwa la mseto, lililokuwa refu kama risiti ya hospitali.

Cha kushangaza, baadhi ya utabiri wake ulikuwa kinyume na timu yake.

Kila pasi au nafasi ya kufunga ilipokosa, ilionekana kumkasirisha zaidi, kana kwamba dau lake lilikuwa hatarini.

Hali hiyo ilitufanya sisi watazamaji wengine kutupiana macho kwa wasiwasi.

Mazingira yakawa mabaya na ya kukera.

Tukio hili si la kipekee. Watu wanaofika katika baa hiyo wamekuwa wakionekana kuwa na hasira zaidi, kelele na hata matusi.

Zaidi ya yote, wamekuwa washirika wabaya wa kuangalia mechi. Kutazama soka siku hizi kunahisi kama kukaa katika ukumbi wa kamari.

Mtu mmoja anapigia skrini kelele, mwingine anachambua beti kila sekunde, huku mwingine akiwa amevunjika moyo baada ya kupoteza dau.

Kinachoshangaza zaidi ni kuona mashabiki wakiombea timu pinzani ishinde ili wapate pesa zaidi.

Usiku huo, Liverpool ilishinda. Kama si kamari, shabiki yule angekuwa akishangilia kwa furaha, akipiga makofi na kusherehekea. Badala yake, aliondoka akiwa amekasirika.

Siku hizi, si jambo la ajabu kwa shabiki kuweka dau dhidi ya timu yake, hasa ikiwa timu hiyo inapewa nafasi kubwa ya kushinda.

Hii ni kwa sababu dau kwa timu dhaifu huleta faida kubwa zaidi.

“Kamari ya mtandaoni, hasa ile ya simu wakati mechi inaendelea, imeharibu kabisa ladha ya kutazama soka,” anasema Morris Omullo, shabiki mkubwa wa soka.

“Leo ukiingia baa, watu wengi wanashughulika kufuatilia dau zao badala ya kufurahia mchezo.”

Hali hii ilijitokeza tena wiki mbili zilizopita wakati Arsenal ilipokutana na Manchester City katika kombe la Carabao Cup.

Rafiki mmoja alikuwa ameweka dau la Sh2,000 kwamba Erling Haaland angefunga bao la kwanza.

Dau lake liliporomoka mapema, na hali yake ikawa ya huzuni, ikiharibu furaha ya wengine waliokuwa wakifurahia mechi.

Zamani, baa zilikuwa mahali pa furaha ambapo mashabiki walijadili soka kwa utulivu. Leo, zimegeuka kuwa maeneo baridi ambapo mazungumzo mengi ni kuhusu dau na tiketi za kamari.

“Ni kama mechi yenyewe haina maana tena,” anasema Brian Muigai.

“Watu wanakasirika kwa sababu wanataka kudhibiti matokeo ya mchezo kutokana na dau waliloweka.”

Tatizo hili halijawaathiri mashabiki pekee. Wachezaji pia wanapata shinikizo. Katika makala ya Sports Illustrated, mchezaji wa Detroit Lions David Montgomery alikiri kuwa aliwahi kuwa na mawazo ya kujiua kutokana na ujumbe mbaya kutoka kwa mashabiki.

Simu zimeongeza kasi ya tatizo hili kwa kufanya kamari iwe rahisi, ya haraka na yenye taarifa nyingi. Watu sasa wanafuatilia takwimu, majeraha ya wachezaji na dau kwa wakati halisi.

Utafiti wa Chuo Kikuu cha Bristol ulionyesha kuwa zaidi ya matangazo 27,000 ya kamari yalionekana mwanzoni mwa msimu wa 2025/26 wa Ligi Kuu Uingereza.

Matangazo hayo yalionekana kwenye televisheni, redio, mitandao ya kijamii na hata viwanjani.

Kwa jumla, kamari imebadilisha namna mashabiki wanavyotazama na kufurahia soka.

Mchezo ambao ulikuwa burudani sasa unageuka kuwa uwanja wa hesabu, hasira na tamaa ya pesa.

Yote haya yanaambatana na ongezeko la matumizi ya takwimu, huku baadhi ya mashabiki wakijikita zaidi katika ufundi na uchambuzi wa kina wa mchezo.

Baadhi sasa huingia viwanjani au kwenye baa wakiwa na karatasi za data, wakifuatilia majeraha ya wachezaji, kuchambua uwezekano wa matokeo kwa wakati halisi, na kufuatilia mechi kadhaa kwa pamoja.

“Wanajua wachezaji wote waliojeruhiwa, na wanajua watakaa nje kwa muda gani, wanachambua hali hata mchezo ukiendelea, kwa kifupi, mchezo sasa si burudani tu,” anasema Morris.