Habari za Kitaifa

Walimu walia SHA inawahujumu wakilazimika kulipia matibabu

Na  LYNET IGADWAH April 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WALIMU nchini wanasema wanalazimika kujilipia pesa za matibabu licha ya kulipa bima ya matibabu chini ya Mamlaka ya Afya ya Jamii (SHA) kila mwezi.

Mwezi mmoja baada ya serikali kuahidi kuchapisha na kusambaza bima ya afya kwa walimu, hali imekuwa tofauti kabisa, huku walimu wakikumbana na viwango vipya vya gharama za huduma hospitalini.Viwango hivyo vipya vimewaacha walimu wakilazimika kuongeza fedha zao ili kupata matibabu.

Mwalimu mmoja jijini Nairobi alisema alishtuka baada ya kufanyiwa upasuaji mdogo wa macho katika Hospitali ya Westlands Laser Eye, ambapo alitarajiwa kulipa Sh12,000. SHA ilikubali kulipa Sh4,500 pekee.

“Nilishtuka nilipoambiwa SHA italipa Sh4,500 tu, na nilipojaribu kupiga simu kutafuta msaada nilizungushwa bila majibu,” alisema.

Walimu wanaougua magonjwa ya muda mrefu wamesema hali ni mbaya zaidi. Mwalimu wa Nakuru aliye na shinikizo la damu na kisukari alisema analazimika kulipa dawa zake mwenyewe baada ya SHA kugharimia Sh1,200 pekee.Vyama vya walimu vimekosoa vikali mfumo huo vikitaka mageuzi ya haraka.ili kuwaokoa walimu

.Katibu wa tawi la Nakuru ya chama cha KNUT Antony Gioche alisema walimu wengi wanalazimishwa kulipa fedha taslimu licha ya kuwa na bima.“Kwa wenye magonjwa ya muda mrefu, hali ni mbaya zaidi,” alisema.

Serikali kupitia SHA imesema viwango hivyo ni sehemu ya utekelezaji wa mpango wa matibabu wa watumishi wa umma (POMSF), huku Mkurugenzi Mtendaji wa SHA Dkt Mercy Mwangangi akisema mazungumzo na hospitali mbalimbali yanaendelea ili kuoanisha viwango hivyo.

Hata hivyo, walimu wanasema hakuna mawasiliano ya moja kwa moja kuhusu mabadiliko hayo, jambo linalowachanganya zaidi wanapofika hospitalini.

Katibu wa tawi la Nyandarua la chama cha KNUT Nyandarua Charles Njau alisema mfumo wa sasa hauwezi kufanya kazi, kwani fedha nyingi zinatumika kwa uchunguzi pekee na kubaki kidogo sana kwa matibabu.

Wakati huo huo, Katibu wa tawi la Pokot Magharibi la chama cha KUPPET Alfred Kamuto alisema walimu wengi hawawezi kupata huduma wanapozihitaji na akataka warejeshwe kwa mpango wa Minet uliokuwepo awali.