Mchuuzi aliyepiga guu kilomita 250 kuja Nairobi kutafuta karo ya chuo apata ahadi kadhaa
KWA muda wa miaka 10, Duncan Kibet, mchuuzi wa bidhaa katika Kaunti ya Bomet amekuwa akijaribu kujiunga na chuo kikuu, apate shahada ili kuimarisha hali ya maisha ya familia yake changa.
Licha ya juhudi hizo, Bw Kibet, 27 amekuwa akihangaika kwa kukosa karo.
Alisomea Shule ya Msingi ya Kipkoligo kabla ya kujiunga na Shule ya Tenwek Boys, Kaunti ya Bomet ambako alipata alama ya C+ kwenye Mtihani wa Kitaifa wa Kidato cha Nne (KCSE) mnamo 2015.
Licha ya kupata alama hiyo, hakuweza kujiunga na elimu ya chuo kikuu kutokana na changamoto za kifedha.
Hivi majuzi baba huyo wa mtoto mmoja alitembea kilomita 250 kutoka kijiji cha Kipkoligo, Chamaner Kaunti ya Bomet hadi Nairobi akilenga kupata karo. Hata hivyo, anasema juhudi hizo hazikumletea fedha.
“Mnamo Januari 28, 2026 nilitembea hadi Nairobi kupata karo baada ya kukaa nyumbani kwa miaka 10 wakati ambapo nilifanya kazi za mikono. Ilinichukua siku nne kufika Nairobi ambako marafiki walikuwa wenyeji wangu,” akasema.
Wakati wa safari hiyo alilala kwenye nyumba ya jamaa zake Narok, Ntulele, Mai Mahiu na baadaye kwenye nyumba za msamaria Nairobi.
Kwa wiki tatu akiwa Nairobi, Bw Kibet aliwaomba wahisani wamsaidie kabla ya kurejea Bomet bila pesa za maana za kufadhili masomo yake.
“Bado sijafua dafu katika kupata karo na nawaomba wahisani waje wanisaidie,” akasema.
Kisa chake hivi majuzi kilivutia umma na akasajiliwa kujiunga na Chuo Kikuu cha Mlima Kenya kusomea fasihi ya Kingereza.
Mbunge wake Richard Yegon (Bomet Mashariki) alimlipia Sh71,000 kugharimia masomo ya muhula mmoja pamoja na Sh6,000 za malazi.
Bw Kibet anatarajiwa kujiunga na chuo hicho mnamo Aprili 27 huku makataa ya kujisajili yakiwa ni Aprili 30.
Viongozi kadhaa wameahidi kuwa watamsaidia kufadhili masomo yake lakini wengi bado hawajatuma hela.
Kwa sasa Bw Kibet ana wingu la matumaini kuwa atapata hela za kutosha kusaidia kufadhili elimu yake.