Makala

Mwanasayansi chipukizi anayetengeneza mafuta ya ethanol kutoka kwa maganda ya mananasi

Na RICHARD MAOSI April 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 1

JE, umewahi kufahamu kuwa maganda ya matunda yanaweza kutumiwa kutengeneza malighafi muhimu katika hatua ya ukuaji wa viwanda?

Hii ndiyo hali halisi katika Shule ya Msingi ya Wasichana ya St Marys inayopatikana Kaunti ya Nakuru.

Wanafunzi wa kundi la Sayansi hutengeneza mafuta aina ya ethanol kutokana na maganda ya mananasi.

Uvumbuzi ambao wanaamini si tu wa manufaa kwao bali kwa kizazi kijacho hususan miongoni mwa wanafunzi ambao wanalenga kuzamia kozi ya uhandisi siku zijazo.

Hapa tunakumbana na mwanafunzi Joy Waruguru mwenye umri wa miaka 14 na pia kinara wa wanafunzi klabu ya Sayansi.

Anasema alipata wazo la kutengeneza malighafi hii muhimu kutokana na maganda ya matunda baada ya kubaini kuwa msambao wa taka ni kero kwa wakazi wengi wa mijini.

Aidha, sehemu nyingi za kuuzia vyakula humu nchini hususan sokoni hazina mpangilio madhubuti wa kutupa taka hizi.

Hatua ambayo hatimaye husababisha mrundiko wa takataka na pia kusababisha maradhi ya kuambukizana.

Waruguru anasema kwa ushirikiano mkubwa baina yake, wanafunzi wenzake na pia mwalimu kinara wamegundua kuwa maganda ya mananasi yanaweza kutengeneza mafuta aina ya Ethanol.

Anafafanua kuwa kabla ya kuwasilisha teknolojia hii kwenye maonyesho ya Kisayansi ya kila mwaka kwa shule za Msingi nchini, walipata fursa ya kuwasilisha kwa wanafunzi wenzao.

“Walituhimiza na kututia moyo kutokana na uvumbuzi huu wa kipekee ambao unazingatia kiwango cha juu cha ubunifu,” asema.

Aidha, walipokuwa wakiendelea na mchakato wa kujiandaa kabla ya mashindano waliunda utaratibu wa kusawazisha muda wao wa darasani na ule wa shughuli hii.

Isitoshe, anawahimiza wanafunzi kujiunga na vyama vya Sayansi shuleni mwao ili kutoa suluhu ya kudumu kwa changamoto nyingi zinazolemaza maendeleo nchini.

Anasema hii itakuwa hatua muhimu sana hasa katika sekta ambazo zimekuwa zikikumbana na changamoto tele kila kukicha.