Sababu za Gachagua ‘kumuuzia’ Kalonzo Jicho Pevu
Aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua amesema kuwa upinzani umefikia makubaliano ya pamoja ya kumuidhinisha Mbunge wa Nyali Mohammed Ali kuwania kiti cha ugavana kaunti ya Mombasa kupitia tiketi ya chama cha Wiper Democratic Movement.
Akizungumza na vyombo vya habari vya Pwani Aprili 25, Gachagua alieleza kuwa licha ya Mohammed Ali kuwa mwanachama wa Democracy for Citizens Party (DCP), wamekubaliana na kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka kumpa tiketi hiyo kama mgombea wa muungano wa upinzani katika kinyang’anyiro hicho muhimu.
“Huyu Mohammed Ali ni mtu wangu wa DCP, lakini nimekubaliana na mwenzangu Kalonzo Musyoka kwamba asimame na Wiper hapa Mombasa,” alisema Gachagua.
Kauli hiyo inajiri siku chache baada ya Gachagua kusisitiza kuwa hakutakuwa na kutengeana maeneo ya kisiasa ndani ya muungano wa upinzani, isipokuwa katika miji mikubwa kama Nairobi na Mombasa, ambako wanapanga kuweka mikakati ya pamoja ili kuongeza nafasi ya ushindi.
Hatua ya kumuidhinisha Mohammed Ali inaonekana kama mkakati wa kuunganisha nguvu za upinzani dhidi ya gavana wa sasa wa Mombasa Abdulswamad Sherrif Nassir, ambaye anatarajiwa kutetea kiti chake katika uchaguzi wa 2027.
Hatua hii inaweza kufanya uchaguzi wa ugavana katika kaunti ya Mombasa kuwa mgumu ikizingatiwa kuwa katibu mkuu wa UDA Hassan Omar anakimezea mate.
Wadadisi wa siasa wanasema kuingia kwa Mohamed Ali kwenye mbio hizo kunaweza kubadilisha kabisa mwelekeo wa siasa za Pwani.
Hii ni kwa sababu mazingira ya kisiasa katika Pwani yamebadilika, hasa baada ya kifo cha aliyekuwa Waziri Mkuu wa zamani Raila Odinga, ambaye kwa muda mrefu alikuwa nguzo muhimu ya ushawishi wa kisiasa katika eneo hilo.
Kwa mujibu wa Manyora, Mohammed Ali ni mgombea “wa kutisha” kwa sababu anavunja mtazamo wa muda mrefu kwamba uongozi wa Mombasa lazima uwe wa mzawa wa Pwani.
Aidha, alibainisha kuwa uwepo wa upinzani wenye nguvu Mombasa unamaanisha kuwa Nassir hawezi kujihisi salama kisiasa. Aliongeza kuwa hali ingekuwa rahisi zaidi kwa gavana huyo kama Raila angekuwa bado hai, kwa kuwa alikuwa na ushawishi mkubwa Pwani.
Kulingana na mchambuzi wa siasa za Pwani Paul Katana, hatua ya upinzani kumuunga mkono Mohammed Ali inaashiria mapambano makali ya kisiasa yanatarajiwa Mombasa.