Habari za Kitaifa

Kenya yapokeza usukani wa ulinzi Haiti kwa mataifa mengine magenge yakiwa bado yanatesa

Na NYABOGA KIAGE April 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KIKOSI cha mwisho cha maafisa 150 wa polisi waliotumwa Haiti chini ya Operesheni ya Usalama ya Kimataifa (MSS) kinatarajiwa kurejea nchini hii leo, Jumanne, Aprili 28, 2026.

Maafisa hao walioachwa nyuma kuangazia mchakato wa uhamisho, wamekuwa katika mchakato wa mabadiliko yanayoashiria awamu mpya katika kero ya muda mrefu kuhusu ukosefu wa usalama Haiti.

Kurejea kwao kunafunga ukurasa uliolazimu Kenya kuchukua wajibu usiotarajiwa kuongoza mchakato wa kurejesha utulivu katika taifa lililo maelfu ya kilomita kutoka bara Afrika, huku maswali yakitanda kuhusu kitakachofuata.

Kwa mujibu wa maafisa wanaofahamu suala hilo, kikosi kilichosalia kimeshirikiana kwa karibu na vikosi vipya, kuhakikisha operesheni zinaendelezwa nchini humo ambamo magenge ya kujihami yamedhibiti nyanja nyingi za maisha ya raia.

“Ni kikosi kilichobaki nyuma na kinahusika katika mchakato wa uhamisho, ikiwemo kuelekeza kikosi kipya nyanjani,” alisema afisa mkuu wa Kenya aliyehusika katika operesheni hiyo.

Kama sehemu ya mabadiliko hayo, Kenya imechangia nafasi muhimu kuandaa vikosi vijavyo chini ya kikosi kipya kilichobuniwa kwa jina Gang Suppression Force (GSF), kinachotarajiwa kuchukua usukani wa operesheni.

Maafisa 395 kutoka Chad waliopokewa na kuelekezwa na kikosi cha Kenya baada ya kuwasili, ni miongoni mwa waliowasili nyanjani.

Kikosi cha Kenya pia kilitangamana na wawakilishi kutoka Bangladesh, Mongolia, na Sri Lanka, wote wanaotarajiwa kutuma maafisa wa kikosi kipya.

Uwiano wao unaashiria mabadiliko kutoka operesheni inayoongozwa na Kenya hadi mfumo mpana wa kimataifa.

Aprili 20, 2026, Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi wa Utawala (DIG-APS), Gilbert Masengeli, alizuru Haiti ambapo alitangamana na maafisa wa Kenya ambao wamehusika na misheni ya MSS.

Alipokewa na Kamanda wa MSS, Godfrey Otunge, Balozi wa Amerika, Haiti David Howell, Balozi wa Kenya, Haiti, Noor Gabow na Naibu Waziri wa Kenya, Amerika, Robert Wasike.

Maeneo makubwa ya jiji kuu la Port-au-Prince, yamesalia chini ya udhibiti wa magenge yaliyojihami vikali, huku serikali ikidhoofishwa na huduma za kimsingi kutatizwa vibaya.

Kiini cha machafuko hayo ni Viv Ansanm, muungano wenye ushawishi mkubwa unaolaumiwa kwa misururu ya mashambulizi dhidi ya miundomsingi muhimu na usalama kuzorota.

Muungano huo uliobuniwa mwishoni mwa 2023 chini ya ushawishi wa kiongozi wa genge sugu, Jimmy Chérizier, uliunganisha makundi hasimu ya kujitenga ikiwemo G9 Family na G-Pep, kuunda mtandao madhubuti ambao umelemea asasi dhaifu za Haiti na kuzidi nguvu vikosi vya usalama.