Habari

Mbadi azozana na kamati ya Bunge

Na DAVID MWERE May 28th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

WAZIRI wa Fedha John Mbadi alizozana waziwazi na wabunge kuhusu uamuzi tata wa kuondoa mashirika muhimu kutoka Wizara ya Kawi na Petroli na kuhamisha zaidi ya Sh55 bilioni kwa Hazina mpya ya Kitaifa ya Miundombinu (NIF).

Kamati ya Bunge kuhusu kawi ilihoji hatua ya kuhamisha Kenya Electricity Generating Company (KenGen), Kenya Power, Kenya Electricity Transmission Company (Ketraco) na Geothermal Development Company (GDC) hadi NIF bila idhini kamili.

Kamati hiyo inayoongozwa na Mbunge wa Nakuru Town East David Gikaria ilisema hatua hiyo imepunguza kwa kiasi kikubwa bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka wa kifedha wa 2026/2027.

“Kuhamisha mashirika hayo kunaweza kuifanya wizara kubaki bila kazi muhimu huku wafanyakazi wakilipwa bila majukumu,” alisema Bw Gikaria.

Vile vile, Idara ya Petroli pia imeathirika baada ya serikali kuuza asilimia 65 ya hisa zake katika Kenya Pipeline Company kupitia uuzaji wa hisa kwa umma uliokamilika Februari 2026.

Naibu mwenyekiti wa kamati hiyo Lemanken Aramat alihoji iwapo Wizara ya Fedha ilifuata sheria na kupata idhini ya Bunge kabla ya kufanya mabadiliko hayo.