Habari

Wadau waonya kituo cha Ebola kitaathiri utalii

Na KALUME KAZUNGU June 1st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WADAU wa utalii wanahofia sekta hiyo itaathirika vibaya endapo kituo kinachopendekezwa cha karantini ya wagonjwa wa Ebola kitajengwa nchini.

Ujenzi wa kituo hicho unatekelezwa eneo la Laikipia kwa nia ya kuwasitiri raia wa Amerika waliotangamana na wagonjwa wa virusi vya Ebola nchini Jamhuri ya Demokrasia ya Congo (DRC) na Uganda.

Wadau wa utalii walishinikiza mpango huo utupiliwe mbali, wakisema ni hatari kwa ukuaji wa sekta ya utalii ambayo ilifufuka miaka ya majuzi baada ya kupata pigo kutoka kwa ugaidi kisha baadaye janga la Covid-19.
Mwenyekiti wa Chama cha Wamiliki wa Hoteli na Wahudumu wa Upishi nchini (KAHC), Kaunti ya Kilifi, Bi Maureen Obunga, alipinga mpango wa kufungua kituo hicho nchini akisema itasababisha mataifa ya ng’ambo kuweka vizuizi vya safari za raia wao dhidi ya kuzuru Kenya.
“Kenya hutegemea pakubwa utalii kiuchumi. Endapo karantini ya Ebola itajengwa itapaka tope taswira nzuri ya nchi yetu kwamba ni taifa lililoathiriwa na Ebola. Tunahofia hilo litasukuma mataifa ya ng’ambo tunayoyategemea kunogesha utalii kuweka marufuku ya safari za raia wao kuzuru hapa,”
“Hiyo ni kumaanisha utalii Kenya utasambaratika,” akasema Bi Obunga, ambaye pia ni Meneja Mkuu wa hoteli maarufu ya Malindi Ocean Beach Resort and Spa.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Watalii Lamu (LTA), Bi Fridah Njeri, pia alipinga kujengwa kwa karantini hiyo Laikipia akishikilia kuwa sekta ya utalii huzingatia sana utulivu wa akili ili kunoga.

“Hata kama hatuna kesi za Ebola nchini mwetu kwa sasa, kuwepo kwa karantini ya kuhifadhia na kuwatibu wagonjwa tayari ni suala linalotatiza akili.

Tunapinga jambo hilo. Tunahofia watalii walioko Uingereza, Amerika, Italia, Ufaransa na kwingineko watakatiza safari zao punde wakisikia Kenya ikihifadhi hao wagonjwa wa Ebola,” akasema Bi Njeri.

Meneja wa Hoteli ya Bamburi Travelers Beach and SPA, Bw Hilary Siele, alisema mbali na watalii wa kimataifa, hata wale wa ndani kwa ndani pia wataanza kususia kuzuru sehemu kama vile Laikipia na viunga vyake, ikiwemo Maasai Mara kutokana na hofu ya kuambukizwa Ebola.

Bw Siele alisema badala ya kituo hicho kujengwa Kenya, ni bora kielekezwe nchi za DRC na Uganda ambazo ndizo chimbuko halisi la virusi vya Ebola.

“Nasikitika kwamba jimbo kama Mlima Kenya ndilo litakaloathirika zaidi kiutalii endapo Karantini itajengwa Laikipia. Kuna watalii wa kimataifa na hata wale wa ndani kwa ndani ambao wote watakwepa kufika maeneo hayo. Tunakataa ujenzi wa karantini Kenya,” akasema Bw Siele.

Mohammed Kassim, afisa wa muungano wa watembezaji watalii ufuoni kaunti ya Kwale, alisisitiza haja ya serikali kutafuta maoni ya wananchi kwanza kabla ya maamuzi yoyote kuchukuliwa kuhusiana na mpango huo.

Naye mwendeshaji mashua za watalii Shella, Lamu, Bw Ali Omar alihoji kuwa huenda wengi wakapoteza kazi zao endapo Kenya itakubali ujenzi wa karantini ya Ebola Laikipia.

“Hatutaki mahangaiko zaidi kwetu sisi vijana kupoteza ajira endapo karantini itajengwa na nchi za ng’ambo ziishie kutangaza marufuku ya raia wao kuzuru Kenya kwa kuhofia kuambukizwa Ebola,” akasema Bw Omar.