Shutuma zaenea baada ya refarii wa Somalia kunyimwa viza ya kuingia Amerika
SHUTUMA zimetanda baada ya refarii wa haiba barani Afrika kutoka taifa la Somalia kuzuiwa kuingia nchini Amerika kusimamia mechi za Kombe la Dunia linalong’oa nanga kesho.
Aidha, maelfu ya mashabiki kutoka nchi ambazo serikali ya Donald Trump ilipiga marufuku za usafiri au kuwekezea vikwazo vya viza usafiri wamelalamikia kukosa fursa ya kushabikia timu zao wakisema “ni dimba lao (Amerika) si sisi (mashabiki)”.
Omar Artan amekuwa refa wa kiwango cha FIFA (Shirikisho la Soka Ulimwenguni) tangu 2018.
Angekuwa Msomali wa kwanza kuchezesha mechi ya Kombe la Dunia, lakini sasa ameondolewa kwenye orodha ya marefa wa dimba baada ya kuzuiwa kuingia nchini Marekani.
Kombe la Dunia linaanza kesho hadi Julai 19 na litaandaliwa kwa pamoja na mataifa ya Amerika, Canada na Mexico.
Artan, aliyeshinda tuzo ya Refa Bora Mwanamume wa Afrika 2025 kutoka Shirikisho la Soka Afrika (CAF), alizuiwa kuingia Amerika alipotua katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Miami.
Inaripotiwa kuwa kwa sasa yupo nchini Uturuki.
Mamlaka za uhamiaji za Marekani hazikutoa sababu mahususi ya kuchukua hatua hiyo, lakini Somalia ni miongoni mwa mataifa yaliyoathiriwa na marufuku ya usafiri iliyowekwa na utawala wa Rais Donald Trump aliporejea mamlakani Januari mwaka jana.
Baada ya mazungumzo na mamlaka za Marekani, FIFA lilithibitisha kuwa Artan hatashiriki Kombe la Dunia.
FIFA ilisisitiza kuwa haihusiki na masuala ya viza na uhamiaji ya taifa mwenyeji, na kwamba imearifiwa hali ya Artan haitabadilishwa.
Kwa kuwa maskani ya marefa wote 52 na wasaidizi wao 88 watakaosimamia mechi za dimba yako mjini Miami refa Artan hawezi kusafiri siku za mechi kutoka taifa la nje kuingia Marekani.
Shutuma za kuzuiwa kwa Artan zinaongeza sauti ya wakosoaji wa mfumo wa viza wa Marekani katika kombe hili, huku mashabiki kutoka mataifa 11 wakipigwa marufuku au kuwekewa vikwazo vya usafiri wasipate fursa ya kushabikia timu zao.
Iran jana ilisema mgao wake wa tiketi za mashabiki kwa mechi za makundi kuondolewa, siku chache baada ya kulalamika kwamba maafisa muhimu wanaoandamana na wachezaji wa timu ya taifa walinyimwa viza.
Utafiti pia umeonyesha kuwa mashabiki kutoka zaidi ya robo ya mataifa 48 yaliyofuzu kwa dimba wanakabiliwa na vikwazo vya usafiri, masharti magumu ya visa au asilimia kubwa ya maombi yao kukataliwa.
Kwa mujibu wa takwimu za Wizara ya Masuala ya Kigeni ya Marekani, mataifa 11 yaliyofuzu kwa kombe yana zaidi ya asilimia 40 ya viza kukataliwa; miongoni mwa Ecuador (40%), Misri (50%), Haiti (50%), Algeria (50%), Cape Verde (50%), Jordan (50%), Iran (60%), Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (60%), Ghana (60%) na Senegal (70%).