Kimataifa

Trump adai afurahia bei ya juu ya bidhaa

Na MASHIRIKA June 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS wa Amerika, Donald Trump amezua mjadala mkubwa baada ya kusema kuwa “anafurahia mfumuko wa bei” huku gharama ya maisha ikiendelea kupanda duniani kutokana na vita vinavyoendelea kati ya nchi yake na Iran.
Kauli hiyo ilitolewa baada ya takwimu mpya kuonyesha kuwa, bei za bidhaa na huduma nchini Amerika na dunia kwa ujumla zimeongezeka kwa kasi katika miezi ya hivi karibuni. Wataalamu wa uchumi wanahusisha hali hiyo na kupanda kwa bei za mafuta kufuatia mzozo wa kijeshi Mashariki ya Kati.
Trump alitetea kauli yake akisema mfumuko wa bei unaoshuhudiwa sasa ni matokeo ya hali ya muda mfupi inayosababishwa na vita, na kwamba uchumi wa Amerika utaimarika mara tu hali ya usalama itakapoimarika.
Aidha, alisema serikali yake inaendelea kuchukua hatua za kuhakikisha usambazaji wa mafuta hauathiriki licha ya mvutano unaoendelea katika eneo la Ghuba.
Kauli ya Trump imetokea wakati mapigano kati ya Washington Dc na Iran yakizidi kushika kasi. Katika siku za hivi karibuni, pande zote mbili zimekuwa zikishambuliana kwa makombora, ndege zisizo na rubani na mashambulizi ya anga katika kile wachambuzi wanakitaja kuwa mojawapo ya migogoro mikubwa zaidi ya kijeshi kuwahi kushuhudiwa katika eneo hilo katika miaka ya hivi karibuni.
Amerika imefanya mashambulizi dhidi ya vituo vya kijeshi na miundombinu ya ulinzi wa Iran, ikisema hatua hiyo inalenga kudhoofisha uwezo wa Tehran kuendesha mashambulizi dhidi yake na washirika wake katika eneo la Mashariki ya Kati.
Kwa upande wake, Iran imeendelea kujibu mashambulizi hayo kwa kulenga vituo vinavyohusishwa na Amerika katika eneo la Ghuba. Serikali ya Tehran imesisitiza kuwa haitakubali kile inachokitaja kuwa vitisho na shinikizo kutoka Washington.
Mvutano huo umeongeza hofu katika masoko ya kimataifa, hasa kutokana na umuhimu wa Mkondo wa Hormuz, ambao ni njia muhimu ya usafirishaji wa mafuta duniani.
Takriban asilimia 20 ya mafuta yanayouzwa katika soko la dunia hupitia eneo hilo.
Kutokana na hali hiyo, bei ya mafuta imeendelea kupanda huku nchi nyingi zikianza kuhofia kuongezeka kwa gharama za nishati, usafiri na bidhaa nyingine muhimu.
Wataalamu wanaonya kuwa, iwapo vita hivyo vitaendelea kwa muda mrefu, athari zake zinaweza kusababisha mfumuko mkubwa zaidi wa bei za bidhaa duniani.
Wakati huo huo, juhudi za kidiplomasia zinaendelea kufanyika kwa lengo la kuzima mvutano.. Duru za kidiplomasia zinasema mawasiliano ya siri kati ya Washington na Tehran bado yanaendelea licha ya mapigano yanayochacha kwa sasa.
Viongozi wa Umoja wa Mataifa pamoja na mataifa ya Ulaya wamezitaka pande zote mbili kurejea kwenye meza ya mazungumzo kabla ya mzozo huo kugeuka vita vya kikanda.
Huku mapigano yakiendelea na gharama za maisha zikipanda, macho yote sasa yameelekezwa Mashariki ya Kati, ambako hatua zitakazochukuliwa katika siku zijazo zinaweza kuamua hatima ya uchumi wa dunia na usalama wa kimataifa.