Idadi ya wakimbizi duniani yapungua kwa mara ya kwanza ndani ya miaka 10
GENEVA, Uswizi:
IDADI ya wakimbizi duniani ilipungua mnamo 2025 kwa mara ya kwanza katika zaidi ya miaka 10, kulingana na ripoti mpya ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR).
Ripoti hiyo inaonyesha kuwa, watu milioni 41.6 ndio walikuwa wakimbizi mwishoni mwa mwaka 2025.
Kupungua huko kumehusishwa hasa na ongezeko la wakimbizi waliorejea katika nchi zao za asili, hususan Afghanistan, Syria na Sudan.
Hata hivyo, UNHCR imeonya kuwa sehemu kubwa ya waliorejea makwao walifanya hivyo katika mazingira magumu, huku baadhi wakilazimishwa kurejea licha ya vurugu zinazoshuhudiwa katika nchi zao.
Shirika hilo linasema hatua kama hizo zinaweza kusababisha wimbi jipya la watu kuhama makazi yao siku zijazo.
Kamishna Mkuu wa UNHCR amesisitiza umuhimu wa jumuiya ya kimataifa kuendelea kusaidia wakimbizi na kuwekeza katika suluhu za kudumu ili kuhakikisha wanaorejea makwao wanapata usalama na fursa za kujijenga upya.