Tahariri

TAHARIRI: Pesa za Wazee wa Mitaa ni sawa ila zisiwe chambo cha kunasa kura

Na MHARIRI MKUU June 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

HATUA ya serikali kutenga takribani Sh4 bilioni kwa ajili ya kuwalipa Wazee wa Vijiji na viongozi wa Nyumba Kumi inastahili pongezi.

Kwa mara ya kwanza tangu Kenya ijinyakulie uhuru mwaka wa 1963, kundi hili ambalo limekuwa nguzo ya utawala wa mashinani litatambuliwa rasmi kupitia mpango wa malipo ya kila mwezi kuanzia mwezi ujao.

Kwa mujibu wa Rasimu ya Bajeti ya mwaka wa Kifedha wa 2026/27 iliyosomwa bungeni wiki iliyopita na Waziri wa Fedha, John Mbadi, wazee wapatao 110,000 watanufaika kwa hazina hiyo mpya.

Kwa miaka mingi, Wazee wa Vijiji wamekuwa wakifanya kazi muhimu ya kuunganisha wananchi na serikali, kutatua migogoro ya kijamii, kuhamasisha usalama wa jamii na kusaidia katika utekelezaji wa sera mbalimbali bila malipo.

Hivyo basi kutambuliwa kwao ni hatua ya haki iliyochelewa kwa muda mrefu.

Vilevile, mpango huu unaongeza juhudi za serikali za kuimarisha ustawi wa jamii, sambamba na Mpango wa Inua Jamii ambao umekuwa ukiwalipa wazee waliofikisha umri wa miaka 70 kiasi cha Sh2,000 kila mwezi.

Hatua hizi zinaonyesha dhamira ya kutambua mchango wa wazee na kuwapa hadhi wanayostahili katika jamii.

Aidha, serikali ya Kenya Kwanza imekuwa ikitekeleza mipango mingine ya uwezeshaji wa wananchi, ukiwemo mradi wa NYOTA unaolenga kuwapa vijana mtaji wa kuanzisha au kupanua biashara zao.

Juhudi kama hizi ni muhimu katika kubuni nafasi za ajira na kuchochea shughuli za kiuchumi na kujenga matumaini kwa kizazi kijacho.

Hata hivyo, pamoja na uzuri wa mipango hiyo, ni muhimu kuzingatia mazingira ya kisiasa yanayoizunguka.

Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027 unakaribia, hali inayofanya baadhi ya Wakenya kujiuliza iwapo baadhi ya miradi hii inalenga zaidi ustawi wa wananchi au kuvutia kura.

Historia ya siasa za Afrika na hasa Kenya imeonyesha kuwa wakati mwingine rasilimali za umma hutumiwa kama nyenzo za kujijengea umaarufu wa kisiasa.

Serikali inapaswa kuhakikisha kuwa hazina hizi mpya zinasimamiwa kwa uwazi, usawa na misingi ya kisheria ili zisionekane kama zawadi za kisiasa kutoka kwa chama au kiongozi fulani.

Wananchi nao wanapaswa kutambua kuwa fedha za miradi kama hii zinatokana na kodi zao.

Hivyo, hazipaswi kutumiwa kama chambo cha kuvutia kura bali kama haki ya wananchi kupata huduma na uwezeshaji kutoka kwa serikali yao.

Kwa hivyo, tunapoipongeza serikali kwa kutambua mchango wa Wazee wa Vijiji na kuanzisha hazina mpya ya kuwalipa, tunasisitiza kuwa mipango hiyo idumishwe kama sera za maendeleo ya kitaifa zinazowanufaisha Wakenya wote, badala ya kugeuzwa kuwa zana za ushindani wa kisiasa kadri uchaguzi wa 2027 unavyozidi kukaribia.