Maoni

Tusirushiane lawama kuhusu vurugu shuleni bali tutafute suluhu pamoja

Na BENSON MATHEKA June 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KUMEKUWA na maoni tofauti kuhusu chanzo cha ongezeko la vurugu katika shule za upili nchini.

Wapo wanaowalaumu walimu kwa kulegeza nidhamu, wengine wakinyooshea kidole wazazi kwa kushindwa kuwalea watoto wao ipasavyo.

Pia kuna wanaodai kuwa serikali imechangia kwa sera zake, huku wengine wakisema wanafunzi wenyewe wamepoteza maadili.

Hata hivyo, badala ya kurushiana lawama, ni wakati wa wadau wote kuketi pamoja na kutafuta suluhu ya kudumu.

Tatizo la vurugu shuleni haliwezi kuhusishwa na upande mmoja pekee kwa sababu mtoto hukua chini ya ushawishi wa familia, shule na jamii inayomzunguka.

Wazazi wana wajibu wa kuhakikisha watoto wao wanajengewa misingi bora ya maadili na kuwafuatilia hata wanapokuwa shuleni.

Walimu nao wanapaswa kuwa zaidi ya wafundishaji darasani kwa kuwa wao pia ni walezi wanaoweza kutambua mapema mabadiliko ya tabia za wanafunzi na kuchukua hatua zinazofaa.

Kwa upande mwingine, jamii imebadilika kwa kasi kutokana na teknolojia na mitandao ya kijamii.

Vijana wengi hupata maudhui yanayochochea jeuri, matumizi ya dawa za kulevya na tabia nyingine hatari.

Bila usimamizi mzuri, athari zake huonekana ndani ya shule.

Huduma za ushauri nasaha zinapaswa kuimarishwa katika taasisi za elimu ili kuwasaidia wanafunzi wanaokumbana na msongo wa mawazo au changamoto nyingine zinazoweza kuwafanya wachukue hatua za vurugu.

Serikali pia inapaswa kuhakikisha shule zina rasilimali na wataalamu wa kutosha kushughulikia masuala ya afya ya akili na nidhamu.

Ni muhimu kukumbuka kuwa kila mwanafunzi anayehusika katika vurugu ni zao la jamii yetu.

Tukichagua kulaumiana badala ya kushirikiana, tatizo litaendelea kujirudia.

Lakini tukikubali kuwajibika kwa pamoja na kuwekeza katika maadili, mawasiliano na ushauri, tunaweza kurejesha utulivu shuleni.