Ushawishi wa Linda Mwananchi wazua wasiwasi ndani ya Upinzani
KUIMARIKA kwa ushawishi wa kundi la Linda Mwananchi pamoja na kauli zinazotofautiana kutoka kwa baadhi ya viongozi wake kunazidi kuibua maswali kuhusu mwelekeo wa upinzani huku uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2027 ukikaribia.
Kundi hilo, ambalo linaongozwa na Katibu Mkuu wa ODM, Edwin Sifuna, lilianza kama vuguvugu lililolenga kurejesha ushawishi ndani ya chama cha ODM kutoka kwa viongozi wanaoshirikiana na serikali ya Rais William Ruto.
Hata hivyo, baada ya miezi kadhaa ya shughuli za kisiasa kote nchini, limeibuka kuwa mojawapo ya makundi yenye mvuto mkubwa, hasa miongoni mwa vijana.
Umaarufu huo umechochea wito wa baadhi ya viongozi na wafuasi wake kumtaka Bw Sifuna kuwa sehemu ya tiketi ya urais ya upinzani mwaka 2027.
Wafuasi wake wanampamba kama sura mpya katika siasa za Kenya, asiyehusishwa na tawala zilizopita na aliye na uwezo wa kuvutia kizazi kipya cha wapigakura.
Kuibuka kwa jina la Sifuna kunatokea wakati ambapo viongozi wengine wakuu wa upinzani tayari wameonyesha nia ya kuwania urais.
Wanaotajwa wanajumuisha kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, aliyekuwa Naibu wa Rais Rigathi Gachagua, aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiang’i, kiongozi wa DAP-K Eugene Wamalwa, kiongozi wa People’s Liberation Party Martha Karua na aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga.
Aidha, taarifa zinaonyesha kuwa baadhi ya viongozi wa Jubilee wanataka Dkt Matiang’i awe sehemu ya tiketi ya urais ya upinzani, ama kama mgombea mkuu au mgombea mwenza.
Mbunge wa Funyula Wilberforce Oundo, ambaye ni mmoja wa viongozi wa Linda Mwananchi, amesema kundi hilo liko tayari kufanya mazungumzo na makundi mengine ya upinzani ili kuunganisha nguvu dhidi ya Rais Ruto.
Hata hivyo, alisisitiza kuwa Edwin Sifuna lazima awe sehemu ya tiketi ya urais.
“Tuko tayari kuzungumza na kila mwanasiasa wa upinzani isipokuwa Rais Ruto. Lakini kiwango chetu cha chini kabisa ni kwamba mmoja wetu lazima awe kwenye tiketi hiyo, na huyo ni Sifuna. Jina lake lazima liwe kwenye karatasi ya kura ya urais,” alisema.
Kauli hiyo imeongeza mjadala kuhusu nafasi ambayo Sifuna anaweza kutekeleza katika muungano wa upinzani.
Huku baadhi ya viongozi wakimtaka agombee urais, wengine wanaona anaweza kuwa mgombea mwenza katika tiketi itakayounganisha upinzani.
Mbunge wa Saboti Caleb Amisi amesema iwapo Sifuna hatakuwa mgombea urais, basi angependa amuunge Bw Maraga.
“Tunahitaji damu mpya katika siasa za Kenya. Hatuwezi kuendelea kufanya mambo kwa njia ile ile na kutarajia matokeo tofauti. Kama si Sifuna, basi Maraga ndiye anayefaa kupewa nafasi,” alisema.
Hata hivyo, Bw Amisi amekuwa akikosolewa kwa kuonekana kutoa ujumbe unaokinzana kisiasa.
Wikendi iliyopita alihudhuria mikutano ya viongozi wa Muungano wa Upinzani unaoongozwa na Kalonzo na Gachagua katika eneo la Magharibi mwa Kenya.
Akijibu ukosoaji huo, alisema kushiriki kwake hakukuwa ishara ya kumuunga mkono mgombea yeyote bali kulikuwa kuwakaribisha viongozi waliotembelea eneo lake.
“Nilikuwa tu mwenyeji wao katika eneo langu. Bado naamini upinzani unapaswa kuunga mkono sura mpya.”
Kundi la Linda Mwananchi sasa limepanga msururu wa mikutano ya kisiasa katika maeneo mbalimbali nchini.
Mikutano hiyo inatarajiwa kufikia zaidi ya kaunti 24 kabla ya tamko kubwa la kisiasa litakalotolewa Septemba jijini Nairobi.
Gavana wa Siaya James Orengo amesema viongozi wa kundi hilo wanaendelea na mikakati ya kuimarisha shughuli zao za kisiasa katika miezi ijayo.
Kwa mujibu wake, lengo ni kuwasikiliza wananchi na kukusanya maoni kuhusu mwelekeo ambao wanataka upinzani uchukue kuelekea uchaguzi mkuu.
Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi alisema kundi hilo tayari limefanya ziara katika maeneo mbalimbali yakiwemo Nairobi, Kitengela, Busia, Narok, Kakamega, Vihiga, Kisumu, Mombasa na Machakos.
Wikiendi iliyopita, viongozi hao walifanya mkutano mkubwa mjini Thika, ikiwa ni hatua ya kwanza ya kuingia eneo la Mlima Kenya.
Osotsi alisema mikutano mingine imepangwa kufanyika Kisii, Trans Nzoia, Bungoma, Meru, Tharaka Nithi, Kilifi, Kwale, Siaya, Migori na Homa Bay.
Kundi hilo pia linapanga kufanya mkutano Eldoret, mji unaochukuliwa kuwa ngome ya kisiasa ya Rais Ruto.
“Lengo letu ni kusikiliza wananchi na kupata maoni yao kabla ya kufanya uamuzi kuhusu mwelekeo wa kisiasa wa 2027. Mkutano wa Nairobi mwezi Septemba utakuwa muhimu sana kwa sababu hapo ndipo tutatangaza rasmi ajenda yetu,” alisema Osotsi.
Wakati huo huo, mazungumzo kuhusu uwezekano wa ushirikiano kati ya Linda Mwananchi na Muungano wa Upinzani unaoongozwa na Kalonzo Musyoka na Rigathi Gachagua yanaendelea kushika kasi.
Katika mikutano ya hivi majuzi, viongozi wa pande zote mbili wameashiria uwezekano wa kufanya kazi pamoja ili kusimamisha mgombea mmoja wa urais dhidi ya Rais Ruto.
Ingawa Edwin Sifuna hajatangaza rasmi iwapo atawania urais au atatafuta muhula mwingine kama Seneta wa Nairobi, ushawishi wake unaozidi kuongezeka unamfanya kuwa mmoja wa viongozi wanaotajwa sana katika hesabu za kisiasa za upinzani.