Siasa

Kindiki, Gachagua kuviziana Ol Kalou wakazi wakitazamia kuona pambano kali

Na MWANGI MUIRURI, WAIKWA MAINA June 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

UCHAGUZI mdogo wa eneo bunge la Ol Kalou, Kaunti ya Laikipia unaotarajiwa kuandaliwa Julai 16, 2026 umeibuka kuwa mojawapo ya mashindano yanayofuatiliwa kwa karibu zaidi katika eneo la Mlima Kenya.

Ingawa ni uchaguzi wa kujaza nafasi iliyoachwa wazi na kifo cha mbunge, sasa umechukua sura ya vita vya kisiasa kati ya Naibu Rais Kithure Kindiki na mtangulizi wake Rigathi Gachagua kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.

Hata hivyo, viongozi hao wawili wamechagua kutokuwa mstari wa mbele katika kampeni.

Badala yake, wanategemea washirika wao kuendesha kampeni huku wao wakifuatilia kwa karibu kutoka nyuma ya pazia.

Katika kinyang’anyiro hicho chenye wagombea tisa, ushindani unaonekana kuelekezwa zaidi kati ya mgombea wa chama cha United Democratic Alliance (UDA) Muchina Nyaga na mgombea wa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP) Kamau Ngotho, ambaye anaungwa mkono na mrengo wa Bw Gachagua.

Wagombea wengine ni Wilson Kigwa wa Jubilee, Rachel Wangui wa People’s Democratic Party, Mathenge Mwaniki wa Kenya Moja Movement, Abdifatah Hussein wa Federal Party of Kenya, Timothy Kamau wa People’s Renaissance Party, Stephen Wanyoike wa National Liberal Party na Edwin Muchiri wa Party of National Unity.

Kiti hicho kilibaki wazi mnamo Machi 2026 baada ya kifo cha Mbunge David Kiaraho. Katika uchaguzi wa 2022, Kiaraho alishinda kwa tiketi ya Jubilee baada ya kupata kura 24,058 dhidi ya Kamau Ngotho aliyepata kura 19,380 kupitia UDA.

Wachambuzi wa siasa wanasema uchaguzi huo sasa umegeuka kuwa kipimo cha ushawishi wa Profesa Kindiki na Bw Gachagua katika siasa za Mlima Kenya.

Profesa Kindiki anatarajiwa kutumia ushindi wa UDA kuthibitisha kuwa ndiye mrithi wa kisiasa wa Rais William Ruto katika eneo hilo, huku Bw Gachagua akitaka kuonyesha kwamba, bado ana ushawishi mkubwa miongoni mwa wapigakura wa Mlima Kenya licha ya kuondolewa mamlakani.

Kutokana na hali hiyo, masuala ya maendeleo ya eneo la Ol Kalou yameonekana kufunikwa na siasa za kitaifa zinazohusu kauli mbiu za “Wantam” na “Tutam”, ambazo zimekuwa zikitumiwa na pande hasimu za kisiasa.

Mchambuzi wa siasa Mulila Munywoki anasema kampeni hizo zimepoteza mwelekeo wa kushughulikia matatizo halisi ya wananchi.

“Kinachoendelea Ol Kalou ni kelele za kisiasa. Ujumbe unaotolewa unahusu zaidi uchaguzi wa 2027 kuliko changamoto zinazowakabili wakazi wa eneo hilo,” alisema.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka kambi za wagombeaji, viongozi hao wawili wanapokea ripoti za mara kwa mara kutoka kwa timu zao huku wakitoa mwongozo wa kimkakati bila kuonekana hadharani katika kampeni.

Ushawishi wa Profesa Kindiki unaonekana kupitia Mwakilishi wa Wanawake wa Nyandarua Faith Gitau na aliyekuwa Waziri wa Utumishi wa Umma Moses Kuria.

Kwa upande mwingine, Bw Gachagua anategemea Seneta wa Nyandarua John Methu na Mbunge wa Kipipiri Wanjiku Muhia.

Ingawa Gachagua hajafanya mikutano mingi ya hadhara katika eneo hilo, amekuwa akihutubia baadhi ya mikutano kupitia simu kwa kutumia vipaza sauti.

Profesa Kindiki naye amedumisha kimya hadharani huku washirika wake wakiongoza kampeni.

Jumanne, Bw Gachagua alikutana na viongozi kutoka Nyandarua katika makazi yake ya Wamunyoro ambapo uchaguzi wa Ol Kalou ulitajwa kuwa miongoni mwa ajenda kuu za mkutano huo.

Mwenyekiti wa Baraza la Wazee la DCP Maina Kamanda amesema Bw Gachagua anatarajiwa kufanya ziara ya kampeni Ol Kalou siku chache kabla ya Julai 13 ili kuhitimisha shughuli zake za kisiasa kabla ya uchaguzi.

Kwa upande wake, Profesa Kindiki hajatangaza wazi ni lini atajiunga na kampeni, ingawa Bi Gitau amedokeza kuwa kuna uwezekano wa kuzinduliwa kwa miradi ya maendeleo katika eneo hilo.

Miongoni mwa wapigakura, kampeni hizo zimeibua hisia mseto.

Baadhi wanaziona kama nafasi ya kuamua mwelekeo wa kisiasa wa Mlima Kenya, huku wengine wakilalamikia siasa za pesa na ahadi zisizotekelezeka.

Stephen Mungai, mkazi wa Wadi ya Rurii mwenye umri wa miaka 28, alisema kampeni zimejaa fedha, propaganda na ahadi nyingi.

“Pesa zinamiminika kila mahali. Ahadi ni nyingi lakini mwishowe wananchi wanataka kuona matokeo. Tayari watu wamegawanyika kulingana na makundi ya kisiasa,” alisema.